Atakayechoma Moto Hifadhi Ya Vyanzo Vya Maji Jela Miaka Saba
Morogoro, 21 Aprili 2023: Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Bi. Fatma Mwassa amewataka wakazi wa mkoa huo kuwa walinzi na kuheshimu mipaka ya hifadhi ya vyanzo vya maji na kwamba serikali itawachukulia hatua kali za kisheria wale wote watakaohusika na vitendo vya kuchoma moto hifadhi ya vyanzo vya maji ikiwemo kuwafikisha mahakamani kwa mujibu wa sheria.
Ametoa agizo hilo wakati wa uzinduzi wa kampeni ya kupanda miti rafiki ya maji inayotekelezwa na Bodi ya Maji Bonde la Wami na Ruvu ambapo amesema atakayebainika kujihusisha kwa namna yeyote na vitendo vya uharibifu wa mazingira kwa kuchoma moto au kufanya shughuli nyingine za kibanaadamu atachukuliwa hatua ikiwemo kifungo cha miaka saba isiyopungua gerezani.
Amesema katika kuhakikisha eneo linabaki katika uhifadhi tayari mamlaka zimekabidhi jukumu la ulinzi kwa kikosi maalumu cha jeshi la wananchi kwa kushirikiana na jeshi la akiba ambao watakuwepo eneo hilo kwa saa 24.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Maji Bonde la Wami Ruvu Elibarik Mmassy amesema kampeni hiyo inalenga kupanda miti milioni 2 katika maeneo mbalimbali ya vyanzo vya maji katika mkoa wa Morogoro.
Amesema kwasasa bwawa la Mindu linakabiliwa na changamoto ya tope lililochangiwa na shughuli za kibinaadamu kandokando ya bwawa hilo ikiwemo uchomaji wa miti kwajili ya uandaaji wa mashamba hali iliyochangia kupungua kwa kina cha maji na kuathiri upatikanaji wa maji katika Mji wa Morogoro.