The House of Favourite Newspapers

Aussems Ataja Siku Atakayoanza Kumtumia Mburkinafaso

Mbelgiji, Patrick Aussems.

KOCHA Mkuu wa Simba, Mbelgiji, Patrick Aussems, amefunguka kuwa, beki mpya wa kikosi hicho, Zana Coulibaly, ataanza kutumika mzunguko wa pili wa Ligi Kuu Bara.

 

Mbali na hilo, pia kama watafanikiwa kutinga hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika, basi utakuwa muda muafaka kuanza kumtumia beki huyo raia wa Burkinafaso, lakini siyo hivi sasa.

 

Ikumbukwe kuwa, Coulibaly amejiunga na Simba katika kipindi hiki cha usajili wa dirisha dogo ambapo mara ya mwisho alikuwa akiitumikia Asec Mimosas ya Ivory Coast.

Usajili wa beki huyo unaelezwa kuwa ni mbadala wa Shomary Kapombe ambaye hivi karibuni alipata majeraha akiwa na kikosi cha Taifa Stars na atakaa nje ya uwanja kwa muda mrefu.

 

Akizungumza na Championi Jumamosi, Aussems alisema kutokana na sheria kuwabana, hivi sasa beki huyo hawezi kumtumia kwenye michuano ya kimataifa hadi watinge makundi ambapo watapata fursa ya kuingiza majina mapya na lake likiwemo.

 

“Kwa kipindi chote ambacho amefanya mazoezi tangu atue hapa, nimemuona kuwa ni mchezaji mzuri ambaye anauelewa wa haraka na mwenye kujituma uwanjani.

 

“Licha ya hayo yote, lakini siwezi kumtumia hivi sasa katika michuano ya kimataifa kutokana na sheria kutubana, lakini tukitinga hatua ya makundi nitaanza kumtumia.

 

“Huku kwenye ligi watu wataanza kumuona katika mzunguko wa pili kwa sababu hapo atakuwa fiti zaidi na naamini atakuwa msaada mkubwa kwenye timu na kuziba pengo la Kapombe,” alisema Aussems.

Stori: Ibrahim Mussa na Wilbert Molandi

Comments are closed.