The House of Favourite Newspapers

Aussems Awapiga Mkwara Mzito Nyoni, Wawa

KOCHA mkuu wa Simba, Patrick Aussems, amewashukia mabeki wake Muivory Coast Pascal Wawa na Erasto Nyoni kwa kuwaambia kwa msimu huu hataki kuona timu hiyo ikifungwa mabao ambayo yanaiharibia timu hiyo kuondoka bila ya kufungwa kwenye mechi zao.

 

Kocha huyo amezungumza hayo ikiwa ni baada ya timu hiyo kuruhusu bao katika mchezo wao wa kwanza wa Ligi Kuu Bara ambao walicheza na JKT Tanzania wiki iliyopita na kushinda mabao 3-1, katika Uwanja wa Uhuru jijini Dar.

 

Aussems raia wa Ubelgiji amesema kuwa licha ya kushinda kwa mabao matatu katika mchezo huo kwa sasa hataki kuona mabeki wake wakichafua rekodi zao kwa kuruhusu bao la namna yoyote ile kutoka kwa wapinzani wao.

 

“Tunafurahia tunashinda lakini hiyo bado haitoshi hata kidogo. Kwa sasa tunataka kuona tunashinda lakini pia tunalinda lango letu kuona wapinzani hawafungi bao lolote lile. Ninataka kuona jambo hilo likitokea kwenye mechi zetu zinazokuja.

 

“Tunatakiwa kuongeza umakini zaidi kukamilisha suala hilo, sifurahii sana kuona tunashinda lakini mwishoni tunakuja kuruhusu bao upande wetu, kama ikitokea tunashinda basi iwe bila ya kuruhusu bao,” alisema kocha huyo.

Comments are closed.