Azam Yaitahadharisha KMC
KUELEKEA mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya KMC unaotarajiwa kupigwa leo Novemba 21, mwaka huu kwenye Dimba la Uhuru jijini Dar, Kocha Msaidizi wa Azam FC, Vivier Bahati amefunguka kuwa wamejiandaa kuvuna alama tatu.
Azam FC imekuwa na mwanzo mzuri kwenye ligi msimu huu ikifanikiwa kushinda mechi nane kati ya 10 walizoshuka dimbani, huku wakiwa kileleni kwenye msimamo wa Ligi Kuu Bara na pointi zao 25.
Akizungumza na Spoti Xtra, Bahati raia wa Burundi, amesema: “Tunaendelea na maandalizi kwa ajili ya mchezo wetu dhidi ya KMC, tunawaheshimu ni moja ya timu bora, wamekuwa na matokeo bora msimu huu, lakini sisi kama Azam tunaendelea kusimamia malengo yetu ambayo ni kuwa mabingwa msimu huu.
“Hivyo kila mechi kwetu ni fainali na tunapambana kupata pointi zote tatu, ili uwe bingwa ni lazima ushinde mechi zako, kikubwa mashabiki wetu wazidi kutuunga mkono, malengo yetu ni kuwa mabingwa wa ligi msimu huu.”
HUSSEIN MSOLEKA, Dar es Salaam