The House of Favourite Newspapers

Baada ya Bongo Fleva,Belle 9 Kuimba Gospo

Abedinego Damian ‘Belle 9’

MKALI wa R&B pamoja na Muziki wa Bongo Fleva, Abedinego Damian ‘Belle 9’, huwezi kumtenga na wanamuziki wanaokimbilia ukongwe kwenye gemu ya muziki huo, kwani ana zaidi ya miaka kumi akifanya muziki huo ambapo wimbo wake wa mwanzo Sumu ya Penzi, ulipokelewa vizuri kwenye gamu.

Hata hivyo, pamoja na mabonde na milima aliyopitia kwenye gemu ya muziki bado anapambana na hali yake ambapo ametoa wimbo mpya uitwao Dada.

Ni wimbo uliopokelewa vizuri lakini bado unaonekana haujamrudisha Belle 9 kule ambako alikuwa enzi za nyuma kipindi anatoa ngoma kali kama Masogange, Wewe ni Wangu, Vitamin Music na kutisha kwa kolabu nyingi kali.

Bila shaka juu ya hili na mambo kadha wa kadha yanayoendelea kwenye muziki wake, Belle 9 hawezi kukosa jambo la kusema, Star Showbiz limemtafuta na huyu hapa akibonga mawili matatu;

STAR SHOWBIZ: Unafikiri ujio wako wa sasa umepokelewa vile unavyostahili?

BELLE 9: Ndiyo, mi naona mapokezi ni makubwa kiukweli. Unajua unapofanya kazi halafu inapokelewa vizuri mtaani, ni jambo la kujivunia sana, ujio huu ninaufananisha na wa Sumu ya Penzi ingawa nimekuwa ninapokea maoni kwamba haujapokelewa vizuri, lakini hiyo ni mitazamo ya watu tu.

STAR SHOWBIZ: Unapopokea maoni kama hayo wakati unaamini kazi yako inafanya vizuri unayapokeaje?

BELLE 9: Nayachukulia kwa hali chanya. Unajua kazi zetu zinapokelewa na watu sasa huwa ninatazama yanayosemwa yana ukweli kiasi gani, unajua wakati mwingine watu wanaweza kupindisha ukweli na ukawa uongo.

STAR SHOWBIZ: Kwa muda ambao umekaa kwenye gemu ya Bongo Fleva, ni jambo gani ambalo unahisi hujafanya?

BELLE 9: Kumuimbia Mungu wangu! Nahitaji kutoa wimbo wa dini (Gospo), nikikamilisha hili hakika nitakuwa nimefanya kila kitu kwenye gemu.

STAR SHOWBIZ: Unategemea hilo kulifanya lini?

BELLE 9: Si muda sana. Nikifikia hiyo hatua nitaweka wazi.

STAR SHOWBIZ: Umedumu kwenye gemu kwa zaidi ya miaka 10, nini hasa kinachangia uendelee kuwepo kwenye gemu?

BELLE 9: Ni kufahamu nini cha kufanya kwa wakati gani. Lakini pia kuwa na discipline, kutengeneza ‘network’ na kukomaa kila siku.

STAR SHOWBIZ: Lakini mahali ulipo kwenye gemu unafikiri ndipo unastahili kuwa?

BELLE 9: Hapana, kiukweli ninastahili kuwa mbali sana. Lakini mambo mengine ni ya Mungu, huwezi kujiuliza kwa nini wakati yeye ndiye anapanga kila kitu.

STAR SHOWBIZ: Baada ya kutoka kimuziki, muziki umewahi kukupa wakati mgumu zaidi?

BELLE 9: Ndiyo! Nakumbuka baada ya kutoa nyimbo za mwanzo maisha kidogo yalibadilika na kuwa mazuri, lakini baadaye mambo yalichenji na kuwa mabaya kuliko kawaida.

Nikafulia mbaya. Nikawa siwezi kufanya hata ngoma, Young Dee ndiye alinichukua na kunipeleka studio nikafanya Wimbo wa Amerudi, ndipo maisha yalibadilika tena na kurudi kwenye mstari.

STAR SHOWBIZ: Kutokana na wema huo, kipi ambacho umewahi kumfanyia Young Dee?

BELLE 9: Mambo mengi sana ninafanya naye pamoja, nimshikaji wangu wa nguvu usipime!

STAR SHOWBIZ: Kipi unakiona hakipo sawa kwenye gemu?

BELLE 9: ‘package’ iliyopo kwenye muziki kwa sasa. Mbali na kuwa na sehemu ya biashara kubwa, sehemu hii ya kiki, kiukweli sijui itatufikisha wapi, sioni kama ni njia sahihi sana ya kutumia kwenye muziki. Kuliko kuegemea kwenye kazi.

STAR SHOWBIZ: Unawashauri nini wanamuziki walioibuka kwa sasa?

BELLE 9: Wakaze, lakini wakumbuke kuweka misingi ya kesho ya maisha yao.

Comments are closed.