The House of Favourite Newspapers

Baada ya Dereva Wake Kuuawa, Bobi Wine Akamatwa

Mbunge nchini Uganda Robert Kyagulanyi maarufu kama Boni Wine amekamatwa na polisi saa kadhaa baada ya dereva wake kuuawa kwa kupigwa risasi na polisi akiwa ndani ya gari lake.

 

Mbunge huyo wa Kyadondo aliandika kwenye mtandao wa Twitter kuwa walikuwa eneo linalojulikana kama Arua kwenye kampeni wakati mauaji hayo yalitokea. Uchaguzi mdogo unatarajiwa kuandaliwa eneo hilo Jumatatu katika juhudi za kumtafuta yule atakayechukua nafasi ya mbunge aliyeuawa, Ibrahim Abiriga .

Bobi Wine na viongozi kadhaa wa upinzani walikuwa eneo hilo kumuunga mkono mgombea huru Kassiano Wadri. Mikutano hiyo ilienda vizuri siku yote kabla ya polisi kuanza kukabiliana na wafuasi wa Wadri. Wafuasi wa Wadri nao waliripotiwa kukabiliana na wale wa mgombea wa NRM Tiperu Nusura.

 

Bobi Wine pia aliandika kuwa hoteli yake ilizingirwa na polisi kufuatia visa hivyo. Hata hivyo polisi wanasema kuwa wafuasi wa upinzani watalaumiwa kwa kuuliwa dereva huyo wa Bobi Wine Yasin Kawuma. Msemaji wa polisi Emilian Kayima, anasema watu waliokuwa wamevaa shati za kampeni za mgombea Wadri, walianza kuurushia mawe msafara wa rais hali ambayo ilisababisha polisi kufyatua risasi.

 

“Mwendo wa saa kumi na mbili unusu jioni msafara wa rais ulishambuliwa na wahuni katika manispaa ya Arua wakati rais alikuwa anaondoka uwanja wa Boma ambapo alikuwa amefanya mkutano wa mwisho,” Kayima alisema.

Comments are closed.