The House of Favourite Newspapers

BAADA YA KIFO CHA PATRICK… SIRI NZITO YA MUNA YAVUJA!

SIRI imefichuka kuwa mwigizaji wa filamu za Kibongo, Rose Alfonce Nungu almaarufu Muna Love ambaye hivi karibuni alifiwa na mwanaye, Patrick Peter, inasemekana ana mtoto mwingine kinyume na kauli zake.  

 

Mara kadhaa Muna amenukuliwa akisema kwamba Patrick alikuwa mwanaye pekee, lakini nyuma yake kuna madai kuwa alizaa mtoto mmoja wa kiume (jina linahifadhiwa kimaadili) mwenye umri wa miaka 13.

 

Kwa mujibu wa mmoja wa ndugu aliyezungumza na Ijumaa Wikienda, mbali na Patrick, Muna amezaa na kutelekeza mtoto wa kiume anayesoma darasa la sita katika shule ya …. (jina la shule linahifadhiwa) iliyopo mkoani Kilimanjaro na kwa sasa yupo darasa la sita.

 

Akizungumza na Ijumaa Wikienda, ndugu huyo alimwaga ubuyu kuwa, kitendo cha Muna kutangaza kuhudumia watoto wa watu wengine huku akimuacha mtoto wa kumzaa akiwa analelewa na watu wengine, kinawakwaza ndugu walio wengi. “Tunashangaa sana Muna huwa hamtambulishi kabisa mtoto wake mkubwa na nasikia alisema aliwahi kuzaa mtoto akafa wakati mtoto yupo hai na anatakiwa apate upendo kutoka kwa mama yake.

“Huyo mtoto alizaa na kaka mmoja hivi anaitwa Fredy na alizaliwa mwaka 2005 mwezi 7 katika Hospitali ya Palestina (Sinza, Dar) na walikuwa wanaishi Sinza-Makaburini walikokuwa wamepanga.  “Baadaye Fredy aliamua kuhamia Mkoa wa Morogoro na walikwenda wote (Muna, Fredy na mtoto) na baada ya hapo walirudi kwao Moshi (Kilimanjaro) Kijiji cha Ukaheni wakiwa pamoja.

 

“Baadaye Muna aliamua kwenda Dar kama kusalimia na vitu vyake aliviacha hukohuko (Kilimanjaro) ndipo alipoamua kutokurudi tena Kilimanjaro na hapo ndipo alipokutana na Peter na kufunga naye ndoa kisha wakamzaa marehemu Patrick. “Ilifika kipindi wakaenda Moshi kwa ajili ya kumfanyia Patrick mila za kwao (alipozaliwa) ndipo Muna alipokwenda kuonana na huyo mtoto akiwa na umri wa miaka minne na nafikiri ndiyo ilikuwa mara ya mwisho kuonana naye.

 

“Kinachouma ni kwamba Muna sijui ataishi maisha ya kuigiza mpaka lini ilihali anawasaidia watoto wenye matatizo, hatukatai ni wajibu yeye kusaidia, lakini amwangalie na mtoto wake ambaye alimtoa katika tumbo lake. “Mtoto huwa anawaambia wenzake shuleni kuwa mama yake mzazi ni Muna na wenzake wanamwambia mbona hawajawahi kumuona akija kumwangalia? Mtoto anaishia kulia tu.

 

“Kwa sasa anaishi bweni na analelewa na mama wa kambo ambaye ni mke wa Fredy,” kilidai chanzo hicho. Kwa upande wa Muna alisema kuwa, mtu asipokupenda atakuzushia mambo mabaya ya kila aina. “Unajua mtu asipokupenda kila baya atakuzushia kwa hiyo siwezi kuongelea zaidi kuhusu hilo,” alisema Muna.

 

Alipotafutwa baba wa mtoto huyo Fredy Mmanga aliyepo Kilimanjaro ili aweze kutupa ukweli wa mambo simu yake haikupatikana hewani. Hivi karibuni Muna alihojiwa na gazeti hili ambapo alikana kuwa na mtoto tofauti na Patrick.

STORI:Waandishi Wetu, DAR

Comments are closed.