BAADA ya kufanikiwa kumbakisha mshambuliaji wao Mzimbabwe, Donald Ngoma uongozi wa Yanga umetangaza pigo lingine linakuja kwenye moja ya klabu hapa nchini.
Kauli hiyo, imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Yanga, Hussein Nyika ikiwa ni siku moja imepita tangu wafanikiwe jaribio la Ngoma kwenda kwa watani wao Simba iliyokuwa inamuwania vikali kwa ajili ya kumsajili.
Ngoma alikuwepo kwenye orodha ya wachezaji iliyokuwa inahitajika kwenye usajili wa msimu ujao wa Ligi Kuu Bara
na Kombe la Shirikisho Afrika, mwakani.
Akizungumza na Championi Ijumaa, Nyika alisema bado hawajafunga usajili licha ya kuwasajili nyota watatu ambao ni Abdallah Shaibu ‘Ninja’, Pius Busitwa na Ngoma hivyo wanaendelea kwa ajili kukamilisha ripoti ya kocha wao Mzambia, George Lwandamina.
Nyika amesema hivi sasa wapo kwenye mazungumzo na mchezaji mmoja muhimu ambaye amelificha jina akiamini kama wakifanikiwa kumnasa, basi itakuwa imelamba dume.
Aliongeza kuwa, baada ya kukamilisha usajili wa mchezo huyo ndani ya siku hizi mbili, basi atasafiri nje ya nchi kwa ajili ya kukamilisha usajili wa kiungo mmoja mkabaji wa kimataifa anayecheza namba sita.
“Muda mchache kuanzia leo (jana), kesho (Ijumaa) au keshokutwa tutawataarifu ni mchezaji gani tumemsajili kwenye moja ya klabu kubwa hapa nchini, ninaahidi hilo mimi na kamati yangu ya usajili.
“Baada ya kufanikiwa kumsajili mchezaji huyo, basi haraka nitasafiri kwenda nje ya nchi kwa ajili ya kumfuata mchezaji mwingine wa kimataifa anayecheza nafasi ya kiungo mkabaji, hivyo subiri nitaweka wazi,” alisema Nyika.
Stori: Wilbert Molandi | Championi Ijumaa