Stori: Stephano Mango, Gazeti la Risasi Jumamosi, Toleo la Desemba 31, 2016
RUVUMA: Baba mzazi wa marehemu Denis (26), Sevelin Komba ambaye alifariki baada ya nyoka aliyekuwa amembeba kwenye koti lake kuuawa, ameibuka na kuanika mapya kuhusu tukio hilo lililoteka hisia za wakazi wengi wa Manisapaa ya Songea.
Shughuli ya mazishi ikiendelea.
Denis alifariki dunia Jumanne iliyopita baada ya wananchi kumuua nyoka huyo aliyemsumbua dereva wa bodaboda, Cassian Haule aliyekuwa amempakiza kisha kushtuka baada ya kuguswaguswa na nyoka huyo hivyo kuruka kwenye bodaboda na kupiga kelele za kuomba msaada.
Baba mzazi wa marehemu Denis, Sevelin Komba akizungumza na mwanahabari wetu.
Wananchi walifika eneo la tukio na kumkuta nyoka huyo akiwa chini ndipo walipompiga hadi kumuua na wakati huo, marehemu Denis alionekana kutoka povu kinywani hivyo kukimbizwa Hospitali ya Rufani Mkoa wa Ruvuma lakini akafariki dunia akiwa njiani.
Daktari wa hospitali hiyo, Geofrey Mdede alipomfanyia uchunguzi, alibaini kuwa mwili wa marehemu ulikuwa na sumu ya nyoka licha ya marehemu kutokuwa na jeraha lolote la nyoka mwilini hali ambayo ilizua sintofahamu kwa wananchi.
Nyoka wa marehemu desnis aliyepigwa hadi kufa na wananchi.
Baadhi ya mashuhuda walisema marehemu alikuwa na tabia ya kutembea na nyoka muda mrefu hivyo hawakushangaa kusikia amekutwa akiwa na nyoka kwani wanahisi alikuwa na mambo ya kishirikina.
“Amekuwa akitembea na nyoka mara nyingi hata uwanjani tulikuwa tunamuona sasa tulikuwa tunashindwa kumuelewa, siku ya tukio hatukushtuka kumkuta na nyoka maana ndiyo michezo yake,” alisema mmoja wa mashuhuda ambaye hakupenda jina lake liandikwe gazetini.
Akizungumza na Risasi Jumamosi nyumbani kwake Mateka, baba mzazi wa marehemu alikanusha taarifa hizo kwa kusema mwanaye hajawahi kumuona akiwa na nyoka hata siku moja.
“Si kweli kabisa kuhusu mwanangu kudaiwa kuwa alikuwa anaonekana na nyoka. Sijui hizo taarifa zimetokea wapi, mimi ndiye baba yake, sijawahi kumuona mwanangu akiwa na nyoka hata siku moja,” alisema mzazi huyo.
Wananchi wakielekea kwenye mazishi.
Akimzungumzia nyoka huyo aliyeuliwa na wananchi siku ya tukio, Mhifadhi wa Wanyamapori wa Hifadhi ya Taifa ya Selous Kanda ya Kusini, Msondi Simwanza, alisema ameshangazwa na kuonekana kwake kwani urefu wake ni wa kushangaza.
Alisema kwa uzoefu wake, hajawahi kuona nyoka mwenye urefu mkubwa kiasi hicho (futi 6) katika kanda hiyo.
“Kwa kweli ni wa ajabu, sijawahi kuona nyoka wa aina hii kwa kanda yetu. Imetushtua,” alisema Simwanza.
Marehemu Denis alizikwa Jumatano iliyopita katika Makaburi ya Mateka kwa Mayao ambapo umati mkubwa wa watu ulifurika kwa ajili ya kushuhudia na kushiriki maziko yake huku vijana waliobeba jeneza wakiimba nyimbo mbalimbali na kulikimbiza jeneza kwa mtindo wa mchakamchaka wakisema ‘mkimbize mkimbize nyoka awahi asije kudhuru watu wengine.’
Kwenye mazishi hayo hakuna ndugu aliyeonekana kulia wala hakukuwa na ibada yoyote wakati jina la marehemu linadhihirisha wazi kuwa ni Mkristo lakini alibebwa kwenye jeneza la Kiislamu na kaburi lake lilichimbwa Kiislamu kitu ambacho kiliendelea kuwashangaza wengi.
Gazeti la Risasi Jumamosi, Toleo la Desemba 31, 2016
Comments are closed.