The House of Favourite Newspapers

Baba Ndiku Abariki Irene Uwoya Kuolewa

0
Staa mkubwa wa filamu Bongo, Irene Uwoya.

WAKATI staa mkubwa wa filamu Bongo, Irene Uwoya akirejea nyumbani kutoka Rwanda alikoenda kwa ajili ya kuhani msiba wa mume wake Hamad Ndikumana ‘Ndiku’, baba mzazi wa mwanaume huyo, amebariki mkwe wake kuolewa na mtu mwingine, Risasi Jumamosi linakuwa la kwanza kukujuza.

 

Kwa mujibu wa chanzo chetu kilichokuwepo katika kikao cha mwisho cha kuagana, Mzee Ndikumana alimwambia mama huyo wa mtoto mmoja kuwa anaweza kuolewa, kwani baada ya mwanaye kufariki, anajua upweke atakaokuwa nao.

Baba mzazi wa mwanaume Irene Uwoya, Hamad Ndikumana ‘Ndiku’ akifanya maombi.

“Ninachoweza kukuambia ni kwamba Uwoya sasa yupo huru kuolewa, wazee huku wala hawana tatizo naye, ni yeye tu na kwa jinsi nilivyomuona, anaonekana amefurahi sana kwa tamko hilo,” kilisema chanzo hicho ambacho kipo karibu na muigizaji huyo.

Akizungumza na Risasi Jumamosi juu ya ishu hiyo, Uwoya alikwepa kwenda moja kwa moja, lakini akasema aliagana vizuri na familia ya marehemu mumewe na kuwa baba mkwe wake, alimpa faraja kubwa na kuonyesha wazi upendo wao kwake kwani wanamkubali na hakuwa na matatizo nao tangu akiwa na mumewe.

 

“Jamani alichonifanyia baba yake Ndikumana ni kikubwa sana kwangu, naamini kabisa baraka alizonipa zitanisaidia sana katika maisha yangu kwa sababu hata siku moja sikuwahi kukwazana na familia hiyo na nilikuwa nawaheshimu kama wazazi wangu siku zote” alisema Uwoya.

 

Uwoya alizidi kufunguka kuwa anawashukuru wazazi hao kwa sababu walimpokea vizuri na kumpa heshima zote kama mkwe yeye pamoja na wazazi wake na mtoto wake Krish kitu kilichomfanya kujisikia vizuri sana.

 

“Nilikuwa na majonzi sana lakini kwa jinsi walivyonionyesha ukarimu wao mkubwa, nilijisikia vizuri sana na nilijiona mtu mwingine tofauti kabisa na nilifarijika mno” alisema Uwoya ambaye akiwa huko, mtu wake wa karibu alikuwa ni aliyekuwa mpenzi wa sasa wa Ndiku, Asma.

 

Risasi Jumamosi lilimtafuta mmoja wa watu wa karibu waliosafiri na muigizaji huyo, Mike Sangu ambaye pia ni msanii ambaye alipoulizwa kuhusu ishu ya wakwe kumpa baraka za kuolewa Uwoya, alisema anachokumbuka ni baba mzazi wa Ndiku kumwombea dua, akimtakia safari njema

.

“Hayo mengine mimi siwezi kuyazungumzia, ninachofahamu mzee alimuombea dua na kumtaka aende salama, alimtaka akaendelee na maisha yake, ila asisahau kuikumbuka familia yake, awe anampeleka mtoto Krish huko, walisema wao hawana kinyongo naye kabisa. Walisema tofauti zao na mzazi mwenzake ni mambo ya kawaida katika ndoa, wao hawawezi kuziingilia, ila wanamtambua kama mkwe wao,” alisema Mike.

 

Marehemu Ndikumana alifariki dunia usiku wa Novemba 14, mwaka huu baada ya kuelezwa kuwa jioni yake alikuwa mazoezini na klabu yake ya Rayon Sports, ambako alikuwa ni kocha msaidizi

 

Leave A Reply