MKAZI wa kijiji cha Kilongo, Muheza mkoani Tanga, Saidi Sekizenge (72), amefariki dunia kwa kuteketea kwa moto akiwa shambani kwake. Tukio hilo lilitokea juzi katika kijiji hicho ambako Sekizenge alikuwa anaishi na familia yake.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Edward Bukombe, alisema mzee huyo alifariki dunia kutokana na kuungua na kuteketea wakati akichoma moto majani yaliyokuwa yamekauka shambani mwake.
Alisema wakati akichoma majani hayo, ghafla moto ulimzidi nguvu kutokana na upepo mkali, hivyo kuhamia katika mashamba ya jirani ambayo pia moto ulianza kuyaunguza.
Bukombe alisema baada ya moto huo kusambaa katika mashambaa hayo, Shekizenge alijaribu kuuzima lakini alizidiwa na moshi wa moto na kuzingirwa na moto, na kushindwa kukimbia kutokana na ulemavu aliokuwa nao na hatimaye kuungua mpaka kuteketea kabisa.
Diwani wa Songa wilayani Muheza, Leslie Nchimbi, alisema baada ya tukio hilo, viongozi walitoa taarifa katika kituo cha Polisi Wilaya ya Muheza ambapo polisi na daktari kutoka Hospitali Teule ya Wilaya ya Muheza, walifika eneo la tukio kwa ajili ya uchunguzi kisha kuruhusu mwili uzikwe baada ya uchunguzi.
CREDIT: NIPASHE
Comments are closed.