The House of Favourite Newspapers

Bakteria, Fangasi Wanavyosababisha Wanawake Kutoa Uchafu Sehemu Nyeti

Mwandishi: Mtaalam A. Mandai | IJUMAA WIKIENDA | AFYA

UCHAFU utokao sehemu za siri za mwanamke kutokana na mabadiliko katika mfumo wa homoni unaweza kutoa nafasi kwa vijidudu vya bakteria au fangasi waitwao trikomonia na klamidia kujipenyeza hatimaye kuathiri sehemu hizo. Mara nyingi uchafu huo huwa na rangi tofauti kama ute au uchafu mweupe, njano, kijani au udongo. Uchafu mweupe unaotoka kidogo ni hali ya kawaida lakini ukiwa mwingi na hautoi harufu wala hakuna muwasho, ni hali ya mabadiliko ya homoni na mara nyingi huwatokea wanawake wasiopevusha mayai wanaotumia vidonge vya majira na walioweka kitanzi ili kuzuia

kupata mimba. Hali ikibadilika na kutoa harufu na kuwa na muwasho na uchafu ukawa kama maziwa ya mgando au ukoko wa ugali basi hapo inaashiria mwanamke ana bakteria au fangasi wanaosababisha matatizo hayo. Uchafu wenye rangi ya njano ukiambatana na muwasho na harufu wakati wa tendo la ndoa inaashiria uambukizo ukeni ambao ni wa bakteria na wakati mwingine fangasi.

Kama yatatoka majimaji mepesi sehemu hizo nyeti na yakawa na harufu na muwasho basi uwezekano wa kuwa na uambukizo wa vijidudu vya bakteria pia unakuwepo. Uchafu wa kijani wa usaha unaashiria magonjwa ya zinaa hasa kisonono. Kaswende huendana na vipele au vidonda sehemu za ugonjwa wa malengelenge. Uchafu wa rangi ya udongo mara nyingi unaashiria una

vidonda au mchubuko katika mlango wa kizazi. Hali hii ya kutokwa na uchafu ukeni ikiendana na maumivu wakati wa tendo la ndoa inaashiria mwanamke ana tatizo katika mlango wa kizazi. Ikiwa mwanamke anapata maumivu ya tumbo chini ya kitovu basi inaashiria uambukizo umeshambulia kizazi na hatari yake ni kuziba mirija ya mayai na kutoshika mimba kabisa.

Kifupi ni kwamba wanawake kutokwa na ute mzito wa rangi yoyote sehemu za siri ni tatizo linalohitaji tiba kwani ni kiashiria kuwa ana uambukizo katika mlango wa shingo wa kizazi. Tatizo hili hupata hata watoto wadogo ambao hawajavunja ungo kutokana na hitilafu katika viungo vya uzazi na pia inaweza kusababishwa na matatizo katika mfumo wa vichocheo, yaani hormones.

WANAOPATWA NA TATIZO HILI

Wanawake waliofikia ukomo wa kutoa hedhi hupatwa na hali hii kutokana na kupungua kwa homoni ya estrogen hali inayotokea katika umri mkubwa. Wanawake wanaotumia vitanzi yaani loop kama njia ya uzazi wa mpango na wanaotumia vidonge au sindano kuzuia mimba pia wanaweza kupatwa na hali hii. Kuna wanawake wengi wanajiuliza ni nini chanzo cha tatizo hili? Mwanamke yeyote wa kawaida hutokwa na uchafu kidogo kati ya asubuhi na jioni na hali hiyo kitaalamu huitwa normal vaginal discharge na ni kawaida lakini ikizidi elewa kuwa kuna tatizo.

>>>Itaendelea wiki ijayo.

Comments are closed.