The House of Favourite Newspapers

Bao la Morrison Lirudiwe

0

MASHABIKI wa Simba jana baada ya Bernard Morrison kufunga bao kali dhidi ya Namungo, walilipuka kwa sauti kubwa wakisema: “Bao la Morrison lirudiwe, hatujaliona vizuri.

 

Morrison alifunga bao hilo dakika ya 87 kwa shuti la umbali wa zaidi ya mita 40 akimtesa kipa wa Namungo, Jonathan Nahimana katika ushindi walioupata wa mabao 3-1, mchezo uliochezwa Uwanja wa Majaliwa, Lindi.

 

Simba ilitumia nguvu nyingi kusaka pointi tatu jana baada ya Namungo kutangulia dakika ya 21 kupitia kwa Nzigamasabo Styve.

 

Kuingia kwa bao hilo, kukawapa zaidi presha Simba waliokuwa wakipambana kuhakikisha wanazidi kujitanua kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu Bara.

 

Timu hizo zilienda mapumziko, wenyeji Namungo wakiwa mbele kwa bao 1-0, ndipo Kocha wa Simba, Didier Gomes, akafanya mabadiliko.

 

Mambo yalibadilika kipindi cha pili baada ya Gomes kumtoa Rally Bwalya, nafasi yake ikachukuliwa na Hassan Dilunga na Meddie Kagere alimpisha John Bocco.

 

Chris Mugalu alipachika bao la kusawazisha dakika ya 78 kwa pasi ya Shomari Kaponbe, kisha bao la pili lilipachikwa na Bocco kwa kichwa akimalizia pasi ya Mugalu dakika ya 83.

 

Bocco amekuwa noma kwa siku za karibuni baada ya kupewa nafasi ambapo makali yake yalianza kwenye mechi ya marudiano ya Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Kaizer Chiefs iliyochezwa Uwanja wa Mkapa, Dar, ambapo alifunga mabao mawili kwenye ushindi wa 3-0, lakini Simba ikaondoshwa kwa jumla ya mabao 4-3.

 

Jana wakati Namungo wakiwa kwenye kasi ya kusawazisha bao la pili, Morrison alipachika alimaliza kazi kwa bao hilo tamu ambalo liliwafanya mashabiki wa Simba wasiamini kile wanachokiona kutokana na mazingira aliyofunga wengi kutofikiria kwamba angeweza kufanya hivyo.

 

Simba inazidi kujikita kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu Bara ikiwa na pointi 64 ikicheza mechi 26, huku Namungo ikibaki nafasi ya nane na pointi 40 baada ya kucheza mechi 29.

STORI: ISSA LIPONDA, LINDI

Leave A Reply