The House of Favourite Newspapers

Barbara Ashambuliwa Zanzibar, Akimbilia Polisi

0

MTENDAJI Mkuu wa Klabu ya Simba, Barbara Gonzalez juzi Jumanne usiku alivamiwa na kufanyiwa fujo katika Uwanja wa Amaan, Visiwani Zanzibar muda mfupi baada ya timu hiyo kumaliza kufanya mazoezi uwanjani hapo.

 

Hiyo ikiwa ni siku moja kabla ya mchezo wa fainali wa michuano wa Kombe la Mapinduzi uliopigwa kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar uliomalizika kwa Yanga kuwafunga Simba mabao 4-3 katika hatua ya mikwaju ya penalti baada ya dakika 90 kutoka suluhu.

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Ijumaa, Barbara alifanyiwa fujo hizo wakati akiswali swala ya Insha saa mbili usiku kwenye Uwanja wa Amaan mara baada ya mazoezi ya timu hiyo.“Barbara alivamiwa na kufanyiwa fujo na watu wasiofahamika kabla ya kwenda kutoa taarifa katika kituo cha Polisi cha Zanzibar.

 

“Hivyo, Jeshi la Polisi hivi sasa linawatafuta watu hao waliohusika katika kumvamia na kumfanyia fujo bosi huyo wa Simba,” alisema mtoa taarifa huyo.

Aidha, Barbara alithibitisha hilo kukiri kufanyiwa fujo kupitia kwenye moja ya radio na kusema kuwa: “Wakati naswali walikuja watu wakaanza kunivuta, kunipiga na kuvuta mtandio wangu.

 

“Baada ya tukio hilo niliripoti katika Kituo cha Polisi Ng’ambo nilikofungua jalada lenye namba NGB/RB 247/2021, ambapo watuhumiwa kadhaa walikamatwa na kuwekwa ndani usiku huohuo.”Aidha, Polisi wa kituo hicho walikiri kupokea malalamiko na kufungulia jalada la shambulio la mwisho.

Stori: WILBERT MOLANDI, Dar es Salaam

Leave A Reply