The House of Favourite Newspapers

Beki Matata Yanga Apata Timu Uarabuni

mgomo-yanga Wachezaji wa timu ya Yanga wakifanya maombi na Kocha wao.

Sweetbert Lukonge, Dar es Salaam : Championi Jumatano

BEKI wa kushoto wa Yanga, Haji Mwinyi, yupo mbioni kutaka kuondoka nchini na kwenda kujaribu bahati yake ya kucheza soka la kulipwa nchini Misri ambako amepata ofa hiyo katika moja ya klabu zinazoshiriki ligi kuu ya nchi hiyo.

Dili hilo limekuja ikiwa ni muda mfupi tu baada ya uongozi wa Yanga kudaiwa kumzuia kwenda kufanya majaribio ya kucheza  soka la kulipwa nchini Uturuki ambako alikuwa amepatiwa timu na meneja wa Mbwana Samatta, Jamal Kisongo.

yanga-4

Akizungumza na Championi Jumatano, Mwinyi alisema kuwa hivi sasa yupo katika harakati za maandalizi ya safari ya kwenda Misri kwa ajili ya kwenda kujaribu bahati yake hiyo kwa sababu mkataba wake na Yanga unamalizika mwishoni mwa msimu huu.

Alisema dili hilo ameunganishiwa na kiongozi wa moja ya klabu zinazoshiriki Ligi Kuu Bara ambaye ana mahusiano mazuri na klabu za nchini humo, hivyo kutokana na kuvutiwa na kiwango chake ndipo alipoamua kumtafutia nafasi hiyo.

“Hii ni nafasi nzuri kwangu ukizingatia mkataba wangu na Yanga hivi sasa unaelekea ukingoni, hivyo nitahakikisha naitumia vizuri ili niweze kutimiza ndoto zangu za maisha ambazo ninazo kwa sasa.

“Kiongozi huyo aliyenitafutia nafasi hiyo kusema kweli siwezi kumtaja kwa sasa wala timu ambayo natakiwa kwenda kufanya majaribio mpaka hapo mambo yatakapokuwa yamekaa vizuri kwani si watu wote ambao wanapenda mafanikio ya wenzao,” alisema Mwinyi ambaye pia kuna tetesi kuwa anawindwa kwa udi na uvumba na viongozi wa Simba.

Beki huyo amekuwa mhimili mkubwa kwenye kikosi cha Yanga msimu huu na aliisaidia timu hiyo kufanya vyema kwenye Kombe la Shrikisho Afrika.

 

Comments are closed.