AKICHEZA mechi yake ya kwanza akiwa na Simba, beki mpya Mghana, Lamine Moro inadaiwa amemkosha Kocha Mkuu wa timu hiyo Mbelgiji, Patrick Aussems huku akitamka haoni sababu ya kumuacha nyota huyo katika usajili wake wa Caf.
Simba, tayari imeshusha wachezaji watatu kwa ajili ya kujaribiwa kabla ya kuwasajili katika usajili wa Caf ili kukiimarisha kikosi chao katika Ligi ya Mabingwa Afrika.
Wachezaji hao waliotua nchini ni Mtogo, Hunlede Abel, Sadney Urikhob raia wa Namibia na Moro ambaye yeye tayari amekubalika na Aussems baada ya kuonyesha kiwango kikubwa.
Akizungumza na Championi Ijumaa, Aussems alisema amefurahishwa na kiwango cha beki huyo kwa dakika alizomuona akiwa uwanjani akicheza mchezo wa robo fainali ya SportPesa Cup walipocheza na AFC Leopards ya Kenya.
Aussems alisema wakati beki huyo akiendelea na majaribio hayo, anahitaji muda wa kuendelea kumuangalia mazoezini na kwenye mchezo wa leo watakapokuwa uwanjani wakicheza mchezo wa nusu fainali na Bandari ya Kenya.
“Nimeangalia upigaji wake wa pasi, ukokotaji wake mpira na ukabaji katika kuokoa na kuzuia mashambulizi yupo vizuri Moro, lakini ninahitaji muda wa kumuangalia vizuri.
“Nitamuangalia katika mazoezi yangu ya kila siku na katika mchezo wetu wa nusu fainali tutakaocheza na Bandari, lakini katika mchezo wetu na Leopards alicheza vizuri.
“Lakini kwa upande wa huyu mshambuliaji mpya aliyekuja naye kwenye majaribio ambaye ni Hunlede (Abel), yeye bado hajanifurahisha kiwango chake kwa dakika alizocheza,” alisema Aussems.
Comments are closed.