The House of Favourite Newspapers

Beki Simba anyoosha mikono, adai Ngoma ana roho saba

0

hassanisihaka

Beki wa Simba, Hassan Isihaka.

Sweetbert Lukonge Dar es Salaam
WAKATI mshambuliaji wa Yanga, Mzimbabwe, Donald Ngoma anatua nchini akitokea kwao Zimbabwe baadhi ya mabeki wa Simba walimchukulia kama mchezaji wa kawaida na kudai kuwa hatawasumbua siku watakapokutana naye uwanjani.

Hata hivyo, juzi Jumamosi, mmoja wa mabeki hao wa Simba, Hassan Isihaka ambaye aliwahi kusema kuwa watamdhibiti Ngoma, alishindwa kujizuia na kujikuta akitamka kuwa mshambuliaji huyo wa Yanga ni hatari sana na ana roho saba kama za paka.

Alisema katika mchezo huo wa Ligi Kuu Bara uliochezwa Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam na kumalizika kwa Yanga kushinda mabao 2-0, Ngoma ndiye mshambuliaji aliyewasumbua sana kuliko wengine wote na alikuwa hatari sana kwao.

“Tulijitahidi sana kupambana naye na kumpatia vitisho vingi lakini haikusaidia, jamaa alikuwa anakuja tu, hata haogopi.

“Ilifikia wakati tukaanza kumchezea faulo ili kumpunguza makali lakini haikusaidia, aliendelea na kasi yake hiyo, hakika kwangu mimi huyo ndiye mchezaji aliyetusumbua sana kuliko Amissi Tambwe na huyo Malimi Busungu,” alisema Isihaka na kongeza kuwa jamaa inawezekana ana roho saba kama za paka kwa sababu haogopi.

Hata hivyo, kwa upande wake Ngoma alipoulizwa kuhusiana na upinzani alioupata kutoka kwa mabeki hao, alisema: “Soka siku zote hivyo ndivyo lilivyo, ni mchezo wa kupambana.

“Nawapongeza mabeki hao wa Simba kwa mchezo wao waliokuwa wakinichezea lakini namshukuru Mungu tumeweza kushinda, sijafunga mimi ila wenzangu wameweza kufunga.

“Napenda kuwaambia Wanayanga kuwa nimekuja kufanya kazi na nitapambana kila mechi ili kuhakikisha tunashinda na sitaogopa chochote kile,” alisema Ngoma.

Mechi hiyo juzi ilikuwa ni mechi ya kwanza kwa Ngoma kuitumikia Yanga dhidi ya Simba tangu alipojiunga nayo kwa kitita cha dola 50,000 akitokea FC Platinum ya Zimbabwe. Mpaka sasa ameshaifungia timu yake hiyo mabao matatu msimu huu wa ligi kuu.

Leave A Reply