The House of Favourite Newspapers
gunners X

Benki Ya Absa Tanzania Yaadhimisha Ubunifu Na Ushirikishwaji Kupitia GirlCode Hackathon 2025

0
Mkurugenzi wa Kitengo cha Teknolojia wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Emanuel Mwinuka ( wa nne kushoto) akizungumza na washiriki wa programu iliyopewa jina la ‘Absa GirlCode Hackathon 2025’ ambapo  wanafunzi wa vyuo vikuu wa kike walitakiwa kutengeneza Kodi za kidigitali  zitakazoleta ufumbuzi utakaosaidia  sekta za kibenki pamoja na jamii kwa ujumla. Hafla hiyo ilifanyika jijini Dar es Salaam jana. Kulia kwake ni Mkuu wa Kitengo cha Malipo ya Kibenki ya Absa, Bi. Rose Mwingira.
Benki ya Absa Tanzania imedhihirisha tena dhamira yake ya kuwawezesha wanawake katika teknolojia kupitia kufanyika kwa mafanikio kwa GirlCode Hackathon 2025, shindano la ubunifu lililochukua saa 36 na kuwakutanisha wasichana wabunifu, watengenezaji programu, na wajasiriamali vijana kutoka sehemu mbalimbali za nchi.
Tukio hilo, lililoandaliwa kwa ushirikiano na Women in Tech Centre na Girl Code Africa, liliwapa washiriki jukwaa la kuunda suluhisho za kidijitali zinazoshughulikia changamoto halisi katika nyanja za Teknolojia ya Fedha (Fintech), Akili Bandia (AI), na Usalama wa Mtandao (Cybersecurity).
Akizungumza wakati wa kufunga hafla hiyo jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki, Mkurugenzi wa Rasilimali Watu wa Benki ya Absa Tanzania, Bw. Patrick Foya, aliwapongeza washiriki kwa ubunifu, uthubutu, na uwezo wao wa kutatua changamoto.
“Suluhisho mlizotoa ziliwashangaza si tu kwa ubora wake wa kiteknolojia, bali pia kwa uwezo wake wa kuleta mabadiliko halisi. Mmefanikiwa kushughulikia changamoto ngumu kwa ujasiri na ustadi mkubwa. Mmedhihirisha kuwa ubunifu hauna jinsia, na kwamba mustakabali wa teknolojia ni ang’avu zaidi kwa sababu yenu,” alisema Bw. Foya.
Mkurugenzi huyo alisisitiza kuwa hackathon hiyo haikuwa tu shindano, bali jukwaa la kujifunza, kukua, na kubadilika, ambapo washiriki walishirikiana kubuni suluhisho mbalimbali kuanzia mifumo ya kibenki ya kidijitali hadi injini za uboreshaji zinazoendeshwa na akili bandia, jambo linaloonyesha kuwa wanawake vijana wa Kitanzania wako tayari kuongoza wimbi lijalo la ubunifu wa kiteknolojia.
“Wanawake wanapopewa nafasi, hawashiriki tu, wanaongoza,” aliongeza. “Kizazi kijacho cha viongozi wa teknolojia tayari kipo.”
Akiangazia nafasi ya Absa katika kukuza vipaji vya wanawake, Mkurugenzi huyo alisisitiza kuwa benki hiyo imejikita katika kuunda fursa jumuishi kwa wanawake katika teknolojia, sambamba na dhima ya Absa ya “Kuimarisha Kesho ya Afrika Pamoja, Kisa Kimoja kwa Wakati,” chini ya kauli mbiu “Hadithi Yako Ni Muhimu.”
“Matukio kama haya hayahusu tu uandishi wa programu, bali ni kuhusu kujenga njia endelevu,” alisema. “Tunatambua vipaji, tunalea uwezo, na kufungua milango ya fursa. Absa Bank Tanzania imejizatiti kuhakikisha wanawake vijana waliopata nafasi ya kushiriki leo wanapata fursa za mafunzo, ushauri, na ajira za baadaye.”
Kwa wale ambao hawakupata ushindi, Bw. Foya aliwatia moyo kwa maneno haya: “Kila mtaalamu mkubwa wa teknolojia amewahi kukutana na changamoto. Kinachojalisha ni jinsi unavyokabiliana nazo. Tumia ulichojifunza hapa, endelea kujenga, kuota ndoto, na kuvuka mipaka.”
Mmoja wa washiriki wa shindano hilo, Mariam Saidi Mohammed, mtaalamu wa kutengeneza programu za kompyuta, aliishukuru Benki ya Absa pamoja na GirlCode Hackathon kwa kuandaa tukio hilo, akisema limemsaidia kujenga kujiamini katika kutafuta suluhisho za changamoto mbalimbali kupitia teknolojia.
“Ningependa kuwahamasisha wanawake wote wenye mawazo mbalimbali wasiogope, wajitokeze, wanaweza kutatua matatizo mengi kupitia teknolojia,” alisema Bi. Mariam.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Teknolojia wa Benki hiyo, Bw. Emanuel Mwinuka, alisema kuwa Absa GirlCode Hackathon itasaidia kupunguza pengo la uwiano wa kijinsia katika taaluma ya mifumo ya kompyuta nchini, ambalo limekuwa changamoto katika maeneo mengi ya kazi.
“Changamoto hii haipo tu kwenye sekta ya benki, bali pia katika tasnia nyingine, ndiyo maana sisi Absa tumeamua kuhamasisha wanawake vijana kutoka vyuoni na sehemu za kazi kuchangamkia fursa zilizopo katika ulimwengu wa teknolojia na kuleta suluhisho kupitia teknolojia,” alisema Bw. Mwinuka.
“Tukio la leo limefanikiwa kwa kiasi kikubwa, tumepata washindi watatu, na kwa kuwa tukio hili linafanyika pia katika nchi nyingine, mshindi wa kwanza atapata nafasi ya kushindana na washindi kutoka mataifa mengine kupitia suluhisho zao, ambapo suluhisho bora zaidi litapokea tuzo nyingine,” aliongeza.
Hafla ya GirlCode Hackathon 2025 ilihitimishwa kwa ugawaji wa tuzo, mazungumzo ya mitandao ya kitaaluma (networking), na ahadi ya pamoja ya kuendeleza juhudi za kuwawezesha wanawake katika mfumo wa teknolojia
Leave A Reply