The House of Favourite Newspapers

Biashara Ya Nyeti Bandia Gumzo Bongo – 2

Dar es Salaam: Katika uchunguzi wake wa kina wa wiki kadhaa jijini Dar, Gazeti la Ijumaa lilibaini kushamiri kwa biashara ya nyeti bandia, hasa za kiume ambapo sasa zinauzwa kama njugu na kugeuka gumzo kila kona.

Wiki iliyopita tulieleza jinsi maduka maarufu ya nguo na vipodozi yaliyorundikana hasa maeneo ya Sinza, Kinondoni, Kariakoo na Magomeni jijini Dar, yanavyohusishwa na biashara hii haramu.

 

Katika ufafanuzi wake, Dk Chriss Mauki ambaye ni Mtaalam wa Saikolojia na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, yeye anasema sababu kuu inayowasababisha wanawake kununua viungo hivyo kuwa ni usaliti katika mapenzi hivyo kutafuta unafuu kwa njia hiyo.

“Mwanamke anapoona anasalitiwa kimapenzi, anaona njia bora ni kujimalizia haja zake mwenyewe, kisaikolojia, anahisi ametibu majeraha kwa kujimiliki,” anasema na kuongeza;

 

“Wapo wenye hisia kuwa, kufanya mapenzi mwanamke na mwanaume, ni mfumo dume, hivyo anapopata nyenzo kama hizo, hudhani kuwa ametatua matatizo ya mfumo dume.”

Anasema wanawake kutumia viungo bandia vya kiume kufanya tendo la ndoa, ni suala la kina lenye sababu za kisaikolojia, kikubwa kikiwa ni wanawake kukata tamaa katika mapenzi.

“Ni hatari kwa sababu hali hii inatengeneza kizazi cha watu wasiotoshelezwa na waume zao.

 

“Jambo hili lina madhara makubwa kisaikolojia kwani humfanya mhusika akili yake iwaze au itazame picha mbaya au chafu au kumfikiria kimapenzi mtu asiyekuwepo hapo alipo. Jambo hili ni baya zaidi kwa afya kwani picha hizo haziondoki haraka kichwani mwake tofauti na ushiriki wa tendo la ndoa na binadamu mwenzake moja kwa moja.

 

“Kimaadili inampunguzia heshima, nidhamu na thamani mwanamke anayetumia madude hayo. Mtu anaweza kuwa mzuri kwenye maeneo mengine mengi, lakini akaishia kuwa na matatizo kama hataiacha tabia hiyo mara moja,” anasema Dk Mauki.

 

ALIYEATHIRIKA AFANYEJE?

“Kama bado mhusika anasoma, awe bize na masomo na ajiepushe na makundi hatarishi.

“Ajishughulishe na mazoezi ya viungo kila siku ili kuufanya mwili kutoka jasho na mwili kuimarika.

“Asikae peke yake kwa muda mrefu bila kuwa bize na shughuli yoyote. Kichwa kitupu ni nyumba ya maasi mengi.

“Aepuke vyakula vyenye mafuta mengi na atumie muda mwingi kulala hivyo atakuwa anaipumzisha pia akili yake.

 

“Asipende kujishikashika na mikono sehemu za siri wakati wowote.

“Afute picha zozote chafu iwe kwenye simu au kompyuta yake na asitembelee mitandao yoyote yenye picha hizo. Kama yupo kwenye ‘magroup’ ya namna hiyo kwenye mitandao ya kijamii, basi ajiondoe haraka iwezekanavyo.”

 

Viongozi wa dini wanasemaje? Kwa upande wa Mchungaji na Nabii wa Kanisa la Jerusalem lenye makao yake makuu Kitunda jijini Dar, James Nyakia anasema kuwa jambo hilo ni moja ya matokeo ya mmonyoko wa maadili, watu wanapoacha kufuata sheria na taratibu za Kimungu matokeo yake ni kuibuka kwa matukio ya namna hii.

 

“Kwa mujibu wa mafundisho ya Biblia inapobainika umetenda dhambi kama hiyo hukumu ya watu wa namna ni kwenda motoni.

“Mantiki ni kuwaponya mamilioni ya watu wengine ambao walikuwa na mpango wa kutenda dhambi hii.

“Vijana hawana budi kuoa na kuwatumia wake zao kwa mahitaji ya miili yao hata pia kwa wanawake kuolewa,” anasema Nabii Nyakia.

 

Utafiti kutoka nje ya Tanzania unaonesha kuwa, tatizo hilo la matumizi ya midoli ya ngono lipo kwenye kundi la uraibu wa ngono au ‘sex addiction’ kama ilivyo kwa uraibu wa matumizi ya madawa ya kulevya.

Utafiti uliofanywa nchini Marekani ulibaini kuwa asilimia 39 ya wanawake wenye umri kati ya miaka 18 hadi 60 wanaripotiwa kuwa walishajaribu na wengine wanatumia hadi sasa nyeti bandia za kiume kukidhi haja zao za kingono.

Kwa mujibu wa utafiti huo, baadhi ya wanawake wa rika zote wanajihusisha kwa kiasi kikubwa na tabia hiyo, lakini vijana ndiyo wahusika wakuu.

 

Sababu nyingine ni kunyimwa au kushindwa kutoshelezwa wakati wa kujamiiana na wenza wao.

Kumekuwa na mazoea na usiri mkubwa ndani ya ndoa nyingi huku suala la wenza kuridhishana likiwa la upande mmoja tu wa mwanaume hivyo mwanamke kutafuta njia mbadala ya kujiridhisha.

Hadi kufikia hatua ya mwanamke kutumia nyeti bandia ya kiume, basi ujue anajaribu kutafuta njia mbadala ya kutochepuka au kuomba talaka kama yupo kwenye ndoa.

 

KUNA TIBA?

Unapaswa kujua kuwa, kama wewe ni mwanamke na unajihusisha na matumizi ya nyeti bandia, basi inakufanya uone umepata mteremko wa kutimiza haja zako.

Ukishafikia kwenye hatua hiyo, huo ndiyo unaitwa uraibu na mtu wa aina hii anahitaji msaada wa haraka wa kisaikolojia kutoka kwa wataalam ambapo mhusika ataanza tiba maalum.

Stori: MWANDISHI WETU, Ijumaa

Comments are closed.