The House of Favourite Newspapers

Bila pesa hakuna mapenzi ?

0

PESA ndiyo sabuni ya roho. Pesa ni kichocheo cha furaha. Ukiwa na pesa unajiamimi. Unaweza kufanya unalotaka wakati wowote. Ndiyo maana wengi wanadiriki kusema tafuta pesa ili uwe kama mfalme.

Wanaosema pesa ndiyo kila kitu  wana hoja. Pesa inaweza kukufanya umfurahishe mpenzi wako kwa kumnunulia zawadi. Kumnunulia mapambo ambayo yatamfanya awe na amani kwa wakati husika. Yawezekana kuna vazi alikuwa akilipenda, unapomnunulia, anafurahi.

Unapokuwa hauna kitu ni rahisi kukimbiwa. Ni rahisi mwenzako kukuona huna msaada. Anashuhudia wenzake wanavyofanyiwa na wapenzi wao, anaona yeye ni kama anaishi dunia ya pili. Siyo dunia hii ambayo wenzake wanafurahia mapenzi.

Mapenzi ya kweli yanaweza kupotezwa na pesa kama mtu asipokuwa makini. Pesa ina nguvu. Inaleta uhasama. Inapoteza uaminifu, mtu anaposhawishiwa na pesa, katika mazingira ambayo kwake yeye ni magumu ni rahisi kutumbukia kwenye kishawishi.

Kama mtu anaishi kwenye mazingira ambayo hajui hatima yake, hajui kesho atakula au kuvaa nini ni tatizo. Hapendezi kama wenzake, anaishi kwa masimango.  Akitokea mtu mwenye pesa, akahitaji penzi lake, huyo bila kipingamizi anaanzisha uhusiano pasipo kuangalia ana mpenzi wake au la.

Marafiki zangu, wakati tunatambua umuhimu wa pesa ni vyema tukatanguliza utu kwanza. Mapenzi yana maana pana, pesa isiwalevye. Pesa ina nafasi yake lakini wapendanao mnapaswa kutambua kwamba mapenzi yanahitaji staha.

Upendo wa kweli unabebwa na namna ambavyo wewe unamjali mwenzako. Muonekano wako machoni uwe unamaanisha upendo. Uwe unamaanisha furaha. Furaha yako iwe ni furaha ya mwenzako. Hata kama hamna kitu lakini upendo wa kweli usimame kati yenu.

Mwenzi wako awe ndiyo msiri wako. Tunzianeni siri kadiri muwezavyo. Kama mwenzako hana kitu, mpe moyo wa matumaini. Muoneshe kwamba ipo kesho. Mtatafuta na kupata. Muoneshe njia ya kutafuta pesa ambayo unaijua. Mshauri afanye nini ili aweze kuongeza kipato.

Tengenezeni mazingira tulivu ya kufurahia maisha yenu. Zipo sehemu nzuri ambazo mnaweza kuinjoi bila ya kutumia pesa. Mnaweza kuinjoi maisha kwa kutazama sinema pamoja nyumbani, kwa kula chakula sehemu ambayo haitahitaji kuwa na kipato kikubwa.

Mnaweza kwenda katika fukwe yoyote. Oneni kwamba dunia ya wapendanao ni yenu. Msikubali kuyumbishwa. Mapenzi ya kweli ni hayo mtakayoamua wenyewe kuishi. Msifikiri wenye pesa ndiyo wanaofaidi mapenzi.

Hata hao wenye pesa nao wanateseka. Wana maumivu yao, wanagombana. Hawaoneshani mapenzi ya kweli, wanasalitiana na wanaishi kama vile wako utumwani. Kila mtu anajua lake. Pesa yao haisaidii kuondoa majeraha wanayoyapata kila siku.

Watu wanaishi kama maadui lakini wana pesa ya kutosha benki. Wanalala nyumba moja ya kifahari lakini hawasalimiani hata mwezi mzima. Utajiri wao hautoi ahueni yoyote katika vita yao ya kila siku.

Nyinyi mna amani. Mnaishi katika kipato cha kawaida, msifadhaike. Oneshaneni upendo wa kweli.

Leave A Reply