The House of Favourite Newspapers

Bilionea Kutoka China Atuma Ujumbe Yanga

Kikosi cha timu ya Yanga.

YULE bilionea anayehakikishaga Yanga haipati shida kabisa inapokuwa jijini Mwanza, Yanga Makaga ametuma ujumbe kwa Yanga akisema atawawezesha ili kuhakikisha wanapata ushindi kwenye mchezo wa Kombe la FA dhidi ya Alliance.

 

Makaga ambaye ni mfanyabiashara kwa sasa anaripotiwa kuwa yuko nchini China kwenye mambo yake binafsi. Ikumbukwe kila Yanga inapokuwa na mechi za kanda ya ziwa, Makaga amekuwa akiigharamia kila kitu kwa mapenzi yake hivyo amepanga kufanya hivyo kwenye mechi na Alliance itakayopigwa Machi 30, mwaka huu kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini hapa na bingwa atashiriki Kombe la Shirikisho Afrika.

Katibu mkuu wa Matawi ya Yanga kwa mikoa ya Kanda ya Ziwa, Mhando Madega aliliambia Championi Jumamosi kuwa,yeye na sekretarieti yake wamepokea maelekezo hayo kutoka kwa Makaga ambaye yuko nchini China katika biashara akiwataka wajipange kuhakikisha Yanga inashinda mchezo huo na yeye atawawezesha.

 

“Yanga Makaga ambaye ni mlezi wetu ameniagiza kuhakikisha tunajipanga vizuri ili Yanga iweze kushinda mchezo wetu na Alliance hivyo maandalizi yetu yanaendelea.

 

“Tunatambua ugumu uliopo katika mchezo wetu na Alliance ndiyo maana kiongozi wetu ametuambia tuanze kujipanga mapema na yeye atatuwezesha kwa kila njia ili Yanga iweze kupata matokeo hivyo mpaka sasa tuko mtaani kuhakikisha Yanga inapata ushindi mbele ya Alliance wiki ijayo ili tuweze kusonga mbele,” alisema Madega.

Johnson James, Mwanza

Comments are closed.