MFANYABIASHARA na mdau mkubwa wa soka hapa nchini, Nassor Binslum, kwa muda mrefu amekuwa mwanafamilia wa mchezo wa soka akijitolea kwa kila hali katika mchezo huo, lengo lake likiwa ni kuona soka nchini Tanzania linapiga hatua.
Kampuni yake ya Binslum Tyres Company Limited inayouza vifaa mbalimbali vya magari kama matairi bora aina za Austone ambayo yanavumilia barabara za aina zote zenye vumbi au kokoto pamoja na betri za magari za RB Battery, hivi karibuni amerejea kwenye kikosi cha Coastal Union ya Tanga kitakachoshiriki Ligi Daraja la Kwanza msimu unaotarajiwa kuanza Septemba 16, mwaka huu.
Kurejea kwake kumekuwa faraja kwa timu hiyo iliyopangwa Kundi B, na sasa matumaini yao ni kuona wanacheza Ligi Kuu Bara msimu wa 2018/19.
Mfanyabiashara huyo siku za nyuma aliamua kujiondoa ndani ya klabu hiyo kutokana na kuwa na migogoro mingi, lakini sasa amerejea kwa kazi moja tu, kuisaidia kufanya vizuri na kupanda daraja.
Binslum ambaye kampuni yake inaidhamini timu ya Mbeya City inayoshiriki Ligi Kuu Bara, kwa sasa hana tofauti zozote za kimgongano na viongozi wa Coastal Union kutokana na kumaliza tofauti zao.
Kampuni ya Binslum inakumbukwa mwanzoni mwa msimu wa 2014/15, iliingia mkataba wa udhamini na klabu tatu zilizopanda daraja kucheza ligi kuu kwa msimu huo ambazo ni Ndanda, Mbeya City na Stand United.
Katika udhamini wa timu hizo, ilianza kumwaga mamilioni kwenye Klabu ya Mbeya City kwa kuipa zaidi ya Sh milioni 300 na kuingia nayo mkataba wa miaka miwili ambao ulimalizika Juni, mwaka jana. Kutokana na kubaini kwamba udhamini huo unalipa ndani ya timu hiyo, wakaongeza mkataba mwingine wa miaka miwili wenye thamani ya Sh milioni 300.
Kwa upande wa Stand United na Ndanda, walipewa mkataba wa mwaka mmojammoja, ulipomalizika, hawakuongezewa.
Kabla ya hapo, huko nyuma alikuwa mfadhili wa siku nyingi wa Klabu ya Coastal Union, lakini baadaye akaamua kujiweka pembeni kwa kile kilichoelezwa ni migogoro ya mara kwa mara ambayo ilikuja kusababisha timu hiyo kushuka daraja mwishoni mwa msimu wa 2015/16.
“Kutokana na kuwa mdau mkubwa wa soka hapa nchini, nimeona si mbaya kuzidhamini timu mbalimbali kwa lengo la kuzisaidia kufikia malengo yao.
“Niliwahi kuidhamini Coastal Union, lakini timu hiyo sikuidhamini kwa sababu ya biashara, bali mimi ni shabiki wake na nilikuwa kiongozi kwenye klabu
hiyo hapo zamani, hivyo lengo langu lilikuwa ni kuinua soka kwenye mkoa wangu wa Tanga na klabu yangu niipendayo,” anasema Binslum ambaye hakuwahi kuwa shabiki wa Simba wala Yanga kama ilivyo kwa mashabiki wengi wa soka hapa nchini.
Kutokuwa kwake shabiki wa timu hizo, hakujawafanya Simba na Yanga kuacha kutumia bidhaa zake kwani klabu hizo mara kwa zimekuwa zikinunua matairi imara ya Doublestar kwa ajili ya mabasi yao na kuwasaidia kusafiri salama mikoani wanapoenda kucheza mechi zao.
Hivi karibuni baada ya kurejea, Meneja wa Coastal Union, Hilal Said Hilal, ameliambia Championi Jumatatu kuwa, wameamua kukaa chini na Binsulm pamoja na wadau wengine wawili wa soka ambao ni Salim Pemba na Swedi Mkwabi na kuwaomba kuwapa sapoti katika masuala yote ya maandalizi ya timu yao. Wakakubali.
“Ni kweli katika kipindi cha hivi karibuni, Coastal hatukuwa na mahusiano mazuri wenyewe kwa wenyewe hali ambayo ilisababisha tukashuka daraja kwa aibu.
“Tukaona tulikosea, tukajirekebisha na sasa tupo kwenye maandalizi kabambe ya kuhakikisha tunafanya vizuri katika Ligi Daraja la Kwanza na matumaini yetu ni kucheza ligi kuu msimu wa 2018/19.
“Kitendo cha Binslum na hao wenzake kukubali kutupa sapoti, ni ishara tosha kwamba kwa sasa Wanatanga tumekuwa kitu kimoja, kama ujuavyo ligi tunayoenda kushiriki kama huna fedha za kutosha usitegemee kufanya vizuri, lakini hao wenzetu wamekubali kutusaidia kwa kila kitu, kilichobaki wachezaji kuifanya kazi yao ipasavyo.
“Katika suala zima la usajili, tumefanya kwa umakini, tumeweza kuchukua wachezaji kumi wazoefu ambao waliwahi kucheza ligi kuu kwa muda mrefu akiwemo Hussein Shariff ‘Casillas’ na Athuman Idd ‘Chuji’,” anasema Hilal.
MAKALA-BONGO OMARY MDOSE DAR ES SALAAM
===