The House of Favourite Newspapers

BOBAN HADI RAHA YANGA

DIRISHA dogo la usajili limefungwa usiku wa kuamkia leo na Haruna Moshi ‘Boban’ ni mchezaji wa Yanga.

Masikio inasikika kama masihara lakini ndio ukweli na ndio maana ya dirisha dogo la usajili. Mwezi Julai Spoti Xtra liliripoti usajili wa Boban kwenda Yanga lakini ikashindikana dakika za mwisho.

Lakini juzi Alhamisi alisaini rasmi mkataba wa miezi sita akitokea African Lyon.

 

Kocha wa Yanga, Mwinyi Zahera ameliambia Spoti Xtra linalotoka kila Alhamisi na Jumapili kwamba alimuona Boban kwenye mechi moja tu baina ya Lyon na JKT Tanzania akamuambia mmoja wa viongozi wa Yanga kuwa kiungo huyo ni mchezaji.

Ngoja nikuambie jinsi Boban atakavyoinogesha Yanga;

 

PASI ZA MWISHO

Tangu Ligi ianze msimu huu, Yanga imekuwa ikimtegemea zaidi Ibrahim Ajibu kama mtengenezaji zaidi wa nafasi za kufunga ndio maana anaongoza kwa asisti. Lakini sasa ujio wa Boban utampunguzia kazi.

Umakini wa Boban kwenye kupiga pasi za mwisho, atakuwa msaada mkubwa sana ndani ya Yanga na ni wazi kwamba anaingia moja kwa moja kwenye kikosi cha kwanza kwavile ni chaguo la Kocha.

 

Akiwa African Lyon, Boban alikuwa mpishi mkubwa wa mabao, licha ya wengi kumuona kama amekwisha kutokana na aina ya timu aliyokuwa akichezea ambayo ilikuwa hoi kiuchumi.

 

MAKAMBO ATANOGA

Jambo lingine ambalo Yanga wanaweza kunufaika nalo baada ya kumsajili Boban ni mfungaji bora wa msimu.

Kutokana na umahiri wake wa kutengeneza nafasi nyingi za kufunga, Heritier Makambo ambaye sasa ameshazifumania nyavu mara nane, anaweza kuibuka mfungaji bora msimu huu kwani atakuwa amepata mtu mwingine wa kusaidiana na Ajibu kumtengenezea nafasi za kutumbukiza. Yaani hii inaitwa ushindwe mwenyewe.

 

TAMBWE ATATUPIA SANA

Boban atamrudisha Tambwe kwenye ubora wake wa kuzifumania nyavu kama ilivyokuwa msimu enzi alipojiunga akitokea Msimbazi.

Tambwe alikuwa tishio kwa kuzifumania nyavu kipindi hicho kutokana na kuwa na wapishi wengi wa nafasi za kufunga.

Alikuwa akitengenezewa mara kwa mara na Simon Msuva ambaye sasa anacheza Difaa El Jadid ya Morocco pamoja na Haruna Niyonzima aliyetimkia Simba.

Lakini sasa kutokana na ujio wa Boban kikosini hapo pia unaweza kuwa msaada mkubwa kwa Tambwe ambaye katika siku za hivikaribuni ameanza kurudi kwenye fomu ya kutupia baada ya kupona majeraha.

 

MASHUTI YA MBALI

Ukiachana na uwezo wake wa kutengeneza nafasi za kufunga,Boban anajua kufunga. Ni mahiri sana kwa kufunga mabao ya kupiga mashuti ya mbali ikiwemo mipira iliyokufa.

Akiwa African Lyon msimu huu, yeye ndiye alikuwa mpigaji wa mipira iliyokufa akisaidiana na Mfaransa, Victor Da Costa ambaye kwa sasa aliingia mitini hata bila ya kuaga baada ya kushindwa kuhimili msoto wa Bongo.

 

JINSI BOBAN ATAKA-VYOKUWA AKICHEZA

Boban anafiti katika mfumo wowote ambao Zahera ataamua kumtumia. Anaweza kucheza nyuma ya washambuliaji wawili kama kocha huyo ataamua kuwaanzisha wote Makambo na Tambwe.

Lakini pia anaweza kucheza nyuma ya mshambuliaji mmoja kama Zahera ataamua kumuanzisha Makambo au Tambwe na kuwatengenezea nafasi nyingi za kufunga.

 

“Kusema kweli Boban ni mchezaji mzuri na aliyekomaa na anapokuwa uwanjani hujua nini anacho-kifanya, kwa hiyo naamini atakuwa msaada mkubwa kwetu na kwa timu yetu ya Yanga kwa sababu anajua sana kutengeneza nafasi za kufunga.

 

“Kuhusiana na kuwa na umri mkubwa, hilo siyo tatizo kwani akiwa African Lyon tumeona mambo aliyokuwa akiyafanya, binafsi namuona Boban na injini nyingine ya mabao iliyokuja katika timu yetu.

“Hakika kama Mungu atamjalia uzima, basi Boban lakini pia na sisi sote mimi na Makambo hakika tutawashangaza wengi kwani tutafunga sana na safu yetu ya ushambuliaji itakuwa moto wa kuotea mbali zaidi ya ilivyo sasa,” anasema Tambwe.

Comments are closed.