The House of Favourite Newspapers

Bocco Apewa Tuzo ya Kagere Simba

0

KASI ya kufunga mabao aliyonayo mshambuliaji na nahodha wa kikosi cha Simba, John Bocco imemuibua kocha wake Mtunisia, Adel Zrane ambaye amesema ana imani kubwa mshambuliaji huyo ndiye atakayeibuka na tuzo ya ufungaji bora msimu huu.

 

Bocco ambaye Jumapili iliyopita alifunga bao moja katika ushindi wa mabao 2-0 walioupata Taifa Stars kwenye mchezo wa kimataifa wa kirafiki dhidi ya Malawi, amekuwa na wakati mzuri ndani ya kikosi cha Simba ambapo mpaka sasa ameifungia mabao 13 yanayomuweka katika nafasi ya pili kwenye chati ya wafungaji bora msimu huu nyuma ya Prince Dube wa Azam mwenye mabao 14.

 

Mshambuliaji huyo amefunga mabao saba katika michezo minne mfululizo iliyopita ya michuano mbalimbali, aliyoshuka uwanjani kuichezea Simba na timu ya Taifa Stars.

 

Akizungumza na Championi Jumatano, kocha Zrane alisema: “Vita ya ufungaji bora msimu huu inaonekana kuwa na ushindani mkubwa sana, misimu miwili iliyopita mshambuliaji wetu, Meddie Kagere alitwaa tuzo hiyo mfululizo, lakini msimu huu tayari Dube wa Azam, na Bocco wameongezeka kwenye huo ushindani.

 

“Lakini licha ya kasi aliyonayo Dube mwenye mabao 14, nakuhakikishia kuwa mfungaji bora wa msimu huu atakuwa Bocco kwa kuwa ana kila sababu ya kufanya hivyo, zaidi ya hiyo nina uhakika kuwa Dube atamaliza katika nafasi ya tatu kwani mfungaji bora namba moja na yule wa pili wa ligi watatoka ndani ya kikosi cha Simba.”

STORI: JOEL THOMAS, Dar es Salaam

Leave A Reply