Bodi ya Filamu Yatangaza Filamu Zilizopita Katika Mchujo wa Tuzo za Filamu 2022
DAR ES SALAAM 30 Novemba 2022: Kufuatia ukusanyaji wa filamu kutoka mikoa 25 ya Tanzania Bara ambapo zilikusanywa filamu 840, tarehe 29 Novemba, 2022 Bodi ya Filamu kupitia Katibu Mtendaji wake Dkt. Kiagho Kilonzo imetangaza filamu 189 zilizopita katika mchujo wa awali wa Tuzo za Filamu Tanzania 2022.
Dkt. Kilonzo amesema msimu wa pili wa Tuzo za Filamu Tanzania umekuwa wa mafanikio ukilinganisha na msimu wa kwanza, ambapo mwaka jana zilikusanywa filamu 638 na filamu zilizopita zilikuwa 120 sawa na asilimia 16 ukilinganisha na 189 za mwaka huu sawa na asilimia 23, hivyo kumekuwa na ongezeko la asilimia 4.
Aidha, ameeleza kuwa filamu zilizopita katika mchujo huo zimekuwa na ubora wa hali ya juu katika fani na maudhui, ambapo kazi nyingi zimekuwa na muonekano mzuri wa picha, usikivu mzuri wa sauti, uongozaji mzuri, uigizaji mzuri pamoja nauchaguzi mzuri wa hadithi.
Pamoja na mambo mengine, katibu mtendaji huyo ameeleza kuwa baadhi ya filamu hizo zitaoneshwa na kituo cha Televisheni cha Azam kupitia chaneli ya Sinema Zetu, ambapo tarehe 8 Disemba, 2022 watatangazwa washiriki watakaoingia katika vipengele mbalimbali vitakavyoshidaniwa katika tuzo hizo.
HABARI/PICHA NA BRIGHTON JAMES WA BODI YA FILAMU.