Bondia Hassan Mwakinyo, Mkenya Okwiri Kuzipiga Ubungo Plaza Septemba 29
Ikiwa ni baada ya miaka miwili kupita bondia namba saba Tanzania na namba moja katika uzani wa Super walter nchini, Hassan Mwakinyo anatarajia kupanda ulingoni Septemba 29, mwaka huu kwenye Ukumbi wa Ubungo Plaza, Dar dhidi ya Mkenya, Rayton Okwiri katika pambano la kuwania mkanda wa ubingwa wa mabara wa IBA.
Mwakinyo atapanda ulingoni katika pambano hilo ambalo limeandaliwa na Promosheni ya PAF Promotion ambayo litakuwa ni pambano lao la pili kuandaa tangu waingie rasmi kwenye uandaaji wa mapambano ya ngumi za kulipwa baada ya kuanda pambano la Hata Usipolala Patakucha ambalo lilifanyika Juni 30, mwaka huu kwenye Ukumbi wa Mlimani City kwa Seleman Kidunda kufanikiwa kumchapa kwa pointi Eric Mukadi kutoka DR Congo.
Ikumbukwe mara ya mwisho kwa Mwakinyo kupanda ulingoni katika Jiji la Dar es Salaam ilikuwa ni Septemba 3, mwaka 2021 katika pambano la kimataifa la kuwania mkanda wa Ubingwa wa Afrika ABU dhidi ya Julius Indogo wa Namibia ambaye alimchapa kwa TKO ya raundi ya nne kisha kahamishia shughuli zake nchini Marekani ambapo aliwahi kutoa kauli kuwa hatokuwa na mpango tena wa kupigana ndani ya ardhi Tanzania kabla ya mipango kumuandea tofauti.
Hii itakuwa ni pambano lake pili nchini Tanzania baada ya Aprili 23,. mwaka huu kupanda ulingoni jijini Dodoma dhidi ya Kuvesa Katembo wa DR Congo katika pambano ambalo alishinda kwa pointi baada ya kupita miezi kupita miezi nane tangu apigwe kwa TKO na Liam Smith nchini Uingereza katika pambano lililofanyika Septemba 3, mwaka jana.
Kijiwe cha Ndondi, umejihakikishia kuwa pambano hilo litapigwa kwenye Ukumbi huo wa Ubungo Plaza ambao ndiyo ulikuwa ukumbi ambao Mwakinyo alicheza pambano lake la. mwisho kabla ya kuelekea nchini Marekani.
Kwa upande promota wa pambano hilo, Ally Mndeme alisema kuwa ni kweli wamefikia makubaliano ya pambano hilo kupigwa kwenye Ukumbi wa Ubungo Plaza, Dar ambapo kwa sasa maandalizi yanaendelea vyema kuelekea kwenye pambano hilo.
@ibrahim_musssa