Breaking: JPM Amsamehe Kinana, Membe Atimuliwa Mazima – Video
MKUTANO wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa umemsamehe Katibu Mkuu Mstaafu wa chama hicho, Abdulrahman Kinana, na kumfutia adhabu ya miezi kumi na nane aliyokuwa akiitumikia.
Tangazo hilo limetolewa jijini Dodoma na Mwenyekiti wa CCM Taifa Rais John Magufuli wakati wa kikao cha Halmashauri Kuu ya chama hicho kinachoendelea jijini Dodoma baada ya kuomba ridhaa ya wajumbe wa kikao hicho ambao nao wameridhia Kinana asamehewe.
Rais Magufuli amesema Kinana ameonekana kujutia makosa aliyokuwa ameyatenda na kuomba msamaha, hivyo ni vema akasamehewa ili aungane na wanachama wenzake katika kukijenga chama.
“Mzee wetu Abdulrahman Kinana amekiri hadharani kuwa alifanya makosa, ni uamuzi mgumu kukiri hadharani, alipewa adhabu ya miezi kumi na nane na ameshatumikia miezi minne, hivyo ninawaomba tumsamehe, aje ajiunge nasi, lakini yule mwingine (Bernard Membe) amejitoa mwenyewe.
“Mimi niliomba kura na mzee Pinda na mimi nikampindua, nilikuwa na Makongoro Nyerere lakini leo wote wapo hapa. Sote tuwe kitu kimoja, atakayepatikana ndio tumuunge mkono, maneno mengine yanapitishwa na upinzania na sisi tunayachukua, tusimame na chama chetu,” alisema Magufuli.
Tayari Kinana ametumikia adhabu hiyo kwa muda wa miezi minne na Magufuli ameagiza kesho afike Dodoma ili ajumuike na viongozi wengine wa chama hicho wakiwemo wastaafu katika mkutano wa Kamati Kuu ya CCM Taifa.