Breaking: Nyalandu Atangaza Kurejea CCM Mbele ya Rais Samia -Video
ALIYEWAHI kuwa mwanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Waziri wa Maliasili na Utalii na kisha baadaye kujiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Lazaro Nyalandu ametangaza rasmi kuondoka Chadema kurejea CCM mbele ya Rais wa Tanzania na Mwenyekiti wa CCM Taifa, Samia Suluhu.
Nyalandu ambaye amekuwa Mwenyekiti wa CHADEMA Kanda ya Kati ametangaza uamuzi huo leo Aprili 30, 2021, kupitia Mkutano Mkuu Maalum wa CCM uliofanyika katika Ukumbi wa Jakaya Kikwete, jijini Dodoma akisema ameamua kurejea nyumbani.
“Mh. Mwenyekiti katika nchi ya ugenini wimbo hauiimbiki Mzee Lowassa, Mzee Frederick Sumaye na Mzee Slaa hawa ni mashuhuda wachache kati ya wengi kwanini wimbo wa Bwana hauimbiki katika nchi ya ugenini.
“Mh. Mwenyekiti Watanzania wameiona nyota yako wameguswa na kujawa na furaha na matumaini tele kwa kuinuliwa kwako, ni maombi yetu kwamba mkono hodari wa Mungu ukakuongoze katika safari iliyotukuka ya kuwaongoza Watanzania,” ameongeza Nyalandu.
Nyalandu alitangaza kujiondoa CCM mwaka 2017, aliwania kwenye kinyang’anyiro cha kuteuliwa kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika uchaguzi Mkuu wa mwaka jana 2020 lakini chama hicho kilimpitisha tundu Lissu kupeperusha bendera ya Chadema hivyo Nyalandu alishindwa licha ya maandalizi ya mapema.