Bunge SC Watamba Kunyakua Ubingwa wa Afrika Mashariki

UONGOZI wa Timu ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Bunge Sports Club umetamba kuwa umejiandaa vyema kunyakua Ubingwa wa Mashindano ya Mabunge ya Afrika Mashariki (Inter Parliamentary Games) yatakayoanza kutimua vumbi Disemba Mosi, mwaka huu jijini Dar kwenye Viwanja vya Taifa na Uhuru.

Mashindano hayo yatakayashiorikisha Mabunge ya Nchi za Afrika Mashariki zikiwemo Uganda, Kenya, Sudan Kusini, Rwanda, Burundi na wenyeji Tanzania, huku michezo saba ya soka, gofu, riadha, kuvuta kamba, pete na kutembea kwa mwendokasi ndiyo itashindaniwa.

Akizungumzia juu ya maandalizi yao, Mwenyekiti wa Bunge Sports Club, William Ngeleja amesema kuwa lengo la timu yao ni kuchukua ubingwa wa mashindano hayo ambapo kwa sasa wanaendelea na mazoezi ili kufanikisha suala hilo.
“Tumejiandaa kuhakikisha kwamba tunachukua ubingwa wa Mashindano ya Mabunge, na sasa tunaendelea na mazoezi yetu lakini kwa ajili ya kujiweka sawa,” alisema Ngeleja.
Musa Mateja | GPL.

