Bwalya: Nitapambana Mataji Yaje Simba SC
WAKATI jana Jumapili Simba ikiwa ilianza harakati za kulisaka taji la Ligi Kuu Bara, kiungo wa timu hiyo, Larry Bwalya, raia wa Zambia, amefunguka kuwa atapambana kuhakikisha kikosi hicho kinakuwa na mataji mengi kwa msimu huu.
Kiungo huyo ameongeza kwamba ana shauku kubwa ya kuwa sehemu ya mafanikio ya kikosi hicho kwa kuwa ni moja ya timu kubwa Afrika kwa kipindi hiki.
Bwalya aliyetua Simba kwa mkataba wa miaka miwili akitokea Lusaka Dynamos, tayari ameshatwaa ubingwa wa Ngao ya Jamii na timu hiyo walioutwaa kwa kuifunga Namungo FC.
Kiungo huyo Mzambia ameliambia Championi Jumatatu kuwa kwake atapambana vilivyo kuhakikisha anakuwa moja ya sehemu ya kikosi hicho ambacho kitatwaa mataji mengi kwa msimu huu.
“Tangu nitue hapa Simba najisikia niko nyumbani na nitapambana zaidi kuona timu inafanya vizuri.
“Nina shauku ya kuwa sehemu ya moja ya timu ambayo ilifanya vizuri na kuwa na mafanikio kwa kutwaa mataji kwenye klabu hii ambayo ni moja ya timu kubwa kwa sasa Afrika,” alimaliza Mzambia huyo.
Stori: SAID ALLY,Dar es Salaam