The House of Favourite Newspapers

Caf Yaibadilishia Kambi Simba

0

SIMBA haitarudi tena jijini Dar es Salaam na badala yake itaendelea kupiga kambi mkoani Arusha kwa ajili ya maandalizi ya mchezo wao wa Ligi ya Mabingwa Afrika watakaocheza na Plateau United ya nchini Nigeria.

 

 

Timu hiyo inatarajiwa kucheza mchezo wake wa awali wa Caf kati ya Novemba 27-29, mwaka huu utakaopigwa Nigeria kabla ya kuja kurudiana baada ya wiki moja kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam. Simba juzi ilimaliza mchezo wake wa Ligi Kuu Bara uliochezwa kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid huko Arusha na kufanikiwa kuwafunga Coastal Union mabao 7-0.

 

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Jumatatu na kuthibitishwa na Kocha Mkuu wa timu hiyo Mbelgiji Sven Vandenbroeck kikosi cha Simba hakitarejea Dar na badala yake kitaendelea kubakia Arusha kwa ajili ya kuendeleza na maandalizi ya mchezo huo kabla ya kuondoka keshokutwa Jumatano kuwafuata Wanigeria.

 

 

Mtoa taarifa huyo alisema kuwa kocha Sven ndiye alipendekeza kambi hiyo baada ya kuvutiwa na mazingira ya hali ya hewa ya baridi ambayo ipo Nigeria hivi sasa. “Timu haitarejea jijini Dar na badala yake itaondokea kuelekea Nigeria ikiwa Arusha, kocha ndiye aliyependekeza kambi hiyo iendelee kubakia mkoani huko.

 

 

“Kitu cha kwanza kilichomshawishi kuendelea kubakia huko ni mazingira ya hali ya hewa ya baridi ambayo ipo Nigeria baada ya kupata taarifa ya hali ya hewa ya huko.

 

 

“Kingine ni utulivu wa kambi hiyo ambayo anaamini ni sehemu sahihi kwake ni baada ya kuipendekeza kwani yeye alitaka eneo tulivu kwa ajili ya kufanya maandalizi ya mchezo huo,” alisema mtoa taarifa huo.

 

 

Sven alipotafutwa kuzungumzia hilo alikiri kwa kusema: “Ni kweli timu itaendelea na kambi hapa Arusha, ni baada ya mimi mwenyewe kupendekeza, kwani mkoani hapa ni sehemu tulivu, hivyo timu itaondokea hapa kwenda Nigeria.”

WILBERT MOLANDI, Dar es Salaam

Leave A Reply