LILE Tamasha kubwa la vijana la Victory Campus Night 2019 linatarajiwa kuunguruma leo IJUMAA, MEI 17, 2019 katika Viwanja vya Tanganyika Packers, Kawe jijini Dar ambapo Tamasha hilo linatarajiwa kukutanisha wazungumzaji mashuhuri nchini wa kuwajenga vijana kisaikolojia, wanamuziki mashuhuri wa Muziki wa Injili pamoja na elimu ya kiroho.
Kutoka Afrika Kusini, anatarajia kutua Mkhululi Bhebhe ambaye ameahidi kulipamba tamasha hilo kwa nyimbo zake nzuri.
Mwanamuziki huyo, siku hiyo ataimba nyimbo zake zote zenye kugusa na ujumbe mzuri hivyo watu wafike kwa wingi kumsikiliza yeye pamoja na wanamuziki wengine watakaolipamba tamasha hilo litakaoanza saa 1 usiku hadi majogoo.
“Tanzania yote itasimama siku hiyo kupisha tamasha hilo. Nawaomba mfi ke hapo tuimbe pamoja, tucheze sana mpaka asubuhi tumsifu Mungu kwa ukuu wake,” alisema Bhebhe.
Tamasha hilo lililoandaliwa na Kanisa la Victory Christian Centre Tabernacle lililopo Mbezi Beach jijini Dar, litakuwa na wazungumzaji mashuhuri nchini watakaotoa mafundisho kwa vijana, pamoja na mafundisho ya kiroho yatakayotolewa na mchungaji wa kanisa hilo, Dk. Huruma Nkone.
Wazungumzaji mashahuri wanaotarajia kuzungumza siku hiyo ni Eric Shigongo na Samuel Sasali ambao wataeleza mambo mbalimbali ya msingi kwa vijana kuweza kujitambua, na kujijenga kimaisha.
Mratibu wa tamasha hilo, Jeff Haran amesema tamasha hilo litakuwa ni la aina yake ambapo mbali na wazungumzaji hao, kutakuwa na burudani nzuri kutoka kwa waimbaji binafsi wa nyimbo za injili pamoja na kwaya.
Alisema kwa upande wa waimbaji wa muziki wa Injili mbali na Bhebhe kutoa Afrika Kusini, atakuwepo Upendo Nkone, “Ipyana Kibona na Masanja Mkandamizaji kutoka nyumbani Tanzania.
“Itakuwa ni burudani na elimu ya kiroho na kimwili siku hiyo, watakuwepo pia Rivers of Joy International, Born Kings, Kwaya ya Kijitonyama, TCG Dancers, Mariam Mauki na Kwaya ya Umoja wa Wanavyuo (University Students Mass Choir),” alisema mratibu huyo.
Aidha, mratibu huyo alisema zitakuwepo burudani mbalimbali ambazo zitatolewa kama sapraizi ambazo zitakuwa na mafundisho na kuburudisha.
Alisema Masanja ataonesha komedi kali katika usiku huo hivyo ni vyema watu wakajitokeza kwa wingi kwani siku hiyo itakuwa ni zaidi ya mikesha ya kawaida.
“Itakuwa ni zaidi ya mkesha, tutapata elimu ya kiroho, tutaimba nyimbo za Injili za kusifu na kuabudu. Kutakuwa na madansa ambao wataonesha umahiri wao jukwaani. Hakutakuwa na kiingilio, niwasihi sana vijana mbalimbali kutoka maeneo mbalimbali ya jiji na hata nje ya Jiji la Dar, wafi ke kupata mafundisho na burudani pia,” alisema Jeff.
Comments are closed.