The House of Favourite Newspapers

CCM Yamuonya Maalim Seif Asichafue Viongozi Wake – Video

0

KATIBU wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Humphrey Polepole, amemtaka Maalim Seif Sharif Hamad kuacha kuchafua viongozi wa chama hicho, vinginevyo atashughulika naye.

 

Bila ya kumtaja jina, Polepole amesema ‘mzee yule’ amekuwa na tabia ya kuchafua viongozi wa chama hicho. Polepole ametoa kauli hiyo jana Jumatatu tarehe 31 Agosti 2020, wakati akitaja orodha ya wagombea uwakilishi visiwani humo.

 

“Lakini nataka kutoa rai mzee yule  aache kutaja majina ya viongozi wetu, aache na leo nimetoa heshima kubwa, nimeambatana hapa na wajumbe wenzangu wa Halmashauri Kuu Taifa Bara na Zanzibar ili haya ambayo ninawaeleza ifahamike ndiyo msimamo wa chama chetu,” alisema Polepole.

 

Alisisitiza ni vema akaacha na anajua Chama Cha Mapinduzi wamepiga hatua na itakuwa ngumu kwa vyama vingine kupiga siasa ya kueleweka, wajipange siyo kutengeneza hoja ya kubumbabumba zisizo na mashiko.

 

“Nimehuzunika sana mzee yule kwa sababu anasema uongo kabisa tena hadharani na sina hakika huenda anatafuta namna tumshitaki ili apate kiki kwenye uchaguzi mkuu mwaka huu, hakuna kitu kingine anachotaka zaidi ya kuvuta hisia za watu.

 

“Anataka kutengeneza kitu hivi, kutengeneza umaarufu, sisi hatutafanya hivyo lakini tunamuonya afanye siasa yake, mambo ya CCM atuachie, ziko kauli ambazo Chama Cha Mapinduzi hatuna tatizo nazo zilishakwisha atuache, ni vizuri ajitafakari afanye kazi ambazo zitakuwa na tija.

 

“Wapiga kura wengi ni vijana zaidi na wazee ni wachache, tunasema kwa mkiki huu tunaokwenda nao miaka mitano ya kutekeleza ilani tunakwenda mara tatu zaidi ya miaka mitano iliyopita. Basi ni vizuri tukamaanisha watu, tumekwenda kule Pemba eneo la Mtambwe Taya ambako ndiko anatoka, hajawahi kufanya kitu chochote hata kujenga mnara wa mita moja hajawahi.

 

“Pale Mtwambwe Taya kimejengwa chuo cha ufundi stadi na pale wanafunzi watasoma, kuna shule ya bweni, ziko bweni za kutosha watoto karibu 200 watakaa pale watafundishwa ufundi wa aina mbalimbali. Na mambo hayo yote yamefanyika pale lakini huyu mzee hakufanya chochote, huyu ameshika nafasi ya uandamizi katika serikali hakufanya chochote.

 

“Sasa anatupotezea muda anamsema mgombea wetu, tunasema acha, hii ni mara ya mwisho, tutashughulika na wewe katika namna ambayo inaweza kuleta habari nyingine, fanya kampeni za kistaarabu na sisi tumezindua kampeni juzi, ni nzuri kabisa hatutaki kusema watu, tunasema hoja, tunajenga sababu kwa Watanzania, tumepewa heshima kubwa sana.  Katika miaka mitano tumefanya kazi kubwa, kazi imefanyika kule Zanzibar,” alisema Polepole.

 

Leave A Reply