The House of Favourite Newspapers

Chama ashusha mashine Simba

CLAYTOUS Chama amewaambia viongozi wa Simba kwamba kuna mtu mmoja yuko pale Zesco akitua Msimbazi hali ya hewa itachafuka. Jamaa anatupia hadi aibu. Amewakalisha sehemu akaanza kuwatiririshia faili la jamaa weee jinsi alivyo na akili ya kutupia na kumiliki mpira.

 

Sasa kila muda wakawa wanamwambia tupe namba basi, akawaambia tulieni akaendelea kuwarusha roho tu huku wao wakisisitiza kwamba hiyo biashara imeisha huyo ndio tunayemtaka. Katika yote aliyowaambia yaliyowatisha ni mawili tu.

 

Rekodi yake imeingia kwenye vitabu vya Caf

Huyo straika ameipiga TP Mazembe kwenye Ligi ya Mabingwa msimu uliopita lakini kali zaidi ni kwamba ametupia hat trick ndani ya dakika tano msimu uliopita kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika, Aliwapiga Mbabane Swallows kwao, wale waliotolewa na Simba.

 

Jamaa anaitwa Lazarous Kambole ni Mzambia anaichezea Zesco.

Orlando Pirate na Kaizer Chiefs ziliposikia amepiga hat trick msimu uliopita zikamuibukia uongozi ukawaambia hauizwi mtu hapa. Sasa Simba wanamtaka huyu jamaa kuboresha kikosi chao msimu ujao na hata Mohammed Dewji ‘Mo’ amemuelewa.

 

Sasa Chama akawapa jina na namba.

Habari za uhakika zinasema kwamba Chama aliwapenyezea viongozi jina la Kambole na wameanza
harakati za haraka kumaliza dili lake kwa vile ni miongoni mwa wachezaji lulu wa Ligi ya Zambia. Mchezaji huyo mwenye miaka 25 anavaa jezi namba 7 katika kikosi cha Zesco ya George Lwandamina ambaye ni kocha aliyewaacha Yanga kwenye mataa msimu uliopita kutokana na ukata.

 

Mmoja wa viongozi wa Simba aliiambia Spoti Xtra kwamba dili la mchezaji huyo lazima limalizike kwa vile ni aina ya wachezaji wanaowataka kwa ajili ya michuano ya kimataifa msimu ujao. Alisema kwamba wanatambua ni mchezaji mkubwa ila lazima watumie nguvu kubwa ya fedha kupata wachezaji wazuri wa aina hiyo.

 

Tayari Simba imeshaanza mazungumzo na Mnyarwanda, Jacques Tuysenge wa Gor Mahia ambaye ameonyesha nia pia ya kutua Msimbazi kuungana na pacha wake wa zamani Meddie Kagere.

 

Mo ambaye ameiwezesha Simba kiuchumi kutinga hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu huu, amepania kusuka Simba ya ushindani mwakani huku akisisitiza kwamba malengo yake msimu huu ilikuwa kuingia makundi tu ya michuano hiyo.

WACHEZAJI wa STARS Walivyoondoka KIBABE Uwanjani Baada ya Ushindi

Comments are closed.