The House of Favourite Newspapers

Choo cha akina Diamond aibu

0

No! Wakati supastaa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ akiinjoi maisha kwenye hekalu lake lililoko maeneo ya Tegeta-Madale jijini Dar, habari kutoka nyumbani kwa mama yake mdogo alikozaliwa na kulelewa jamaa huyo Tandale zinadai kuwa choo cha nyumba yao kinamtia aibu.

Habari kutoka kwa majirani waliokerwa na hali hiyo waliolipigia simu gazeti hili zilieleza kuwa choo hicho cha nje kimeharibika, kujaa na kutoa harufu inayohatarisha afya za wakazi wa mtaa huo kutokana na ugonjwa hatari wa kipindupindu unaoenea kwa kasi nchini.

Akizungumza na waandishi wetu, mmoja wa majirani wa nyumba hiyo maeneo ya Tandale-Shule, alisema kuwa choo hicho kiliharibika tangu mwezi uliopita kwa ukuta wake kuangukia nyumba ya pembeni huku shimo la choo likifumuka na kuacha uchafu wazi.

Jirani huyo aliyeomba hifadhi ya jina alisema anashangazwa na jinsi familia hiyo yenye hadhi mjini, inavyopotezea kukarabati choo chao na kuongeza kuwa kwa fedha alizonazo Diamond ishu hiyo inamtia aibu.

“Yaani inashangaza sana, kwa hadhi ya Diamond na fedha alizonazo, anashindwa kuwajengea ndugu zake choo?” alihoji jirani huyo.

Waandishi wetu walishuhudia choo hicho kikiwa kimezungushiwa manailoni huku upande wa chini ukionesha uchafu na harufu kali ikisambaa eneo hilo huku jambo la kushangaza likiwa ni supastaa huyo na mama yake, Sanura Kassim ‘Sandra’ kufika mara kwa mara nyumbani hapo hasa kila anaposhinda tuzo zake za kimataifa na kukikaushia choo hicho.

Akizungumza na waandishi wetu mama Diamond alisema: “Nafahamu choo kina matatizo lakini tumeshampeleka fundi na kuna kipindi alikuwa anasumbua sana lakini kila kitu kipo vizuri na choo kitajengwa muda si mrefu.”

Imeandaliwa na Chande Abdallah, Issa Mnally na Brighton Masalu

Leave A Reply