CRDB Yang’ara Burundi Yatajwa kuwa mkopeshaji mwenye faida kubwa Zaidi
Benki ya CRDB Yang’ara Burundi, Yatajwa Kuwa Mkopeshaji Mwenye Faida Kubwa Zaidi
Benki ya CRDB Tawi la Burundi hatimaye imeibuka kuwa mkopeshaji mwenye faida kubwa zaidi katika nchi hiyo, miaka 11 tangu ilipoingia katika soko la Bujumbura.
Benki hiyo ikiwa na matawi manne nchini Burundi huku pia ikiwa na mpango wa kufungua matawi mengine matatu kwa mwaka huu, ilihusisha mafanikio yake ya muongo mmoja na ubunifu wa usimamizi wake na msaada inaoupata kutoka kwa serikali, kampuni mama na washirika mbalimbali.
Afisa Mkuu wa Fedha wa CRDB (CFO), Frederick Nshekanabo alisema CRDB Burundi imekua na kuwa mkopeshaji mwenye faida kubwa zaidi katika nchi hiyo ambapo ishara zilianza kuonekana mwaka jana baada ya kushika nafasi ya pili.
“Matawi yetu yalifanya kazi kubwa na ya muhimu katika kuimarisha utendaji wa benki yetu nchini, Burundi ikifikia ukuaji wa asilimia 30.7 kwa mwaka katika faida baada ya kodi ya takribani shilingi bilioni 30.2,” Nshekanabo aliwaambia wanahisa hivi karibuni jijini Arusha kwenye Mkutano Mkuu wa 29 wa Mwaka.
CRDB Burundi imeshuhudia mali zake zikikua kwa asilimia 16.4 hadi shilingi bilioni 985 kwa mwaka jana huku amana za jumla zikiongezeka kwa asilimia 3.8 hadi shilingi bilioni 547.3.
Sekta ya benki nchini Burundi ina takriban benki 13 za kibiashara, ikiwa ni pamoja na KCB Burundi, Burundi Commercial Bank, Burundi Bank of Commerce and Investment, Diamond Trust Bank Burundi, Women’s Investment and Development Bank na EcoBank Burundi.
Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Burundi SA, Fredrick Siwale aliwaambia baadhi ya wanahabari katika Mkutano Mkuu wa Mwaka kuwa katika robo ya kwanza ya mwaka huu, tawi hilo lilirekodi faida ya jumla ya faranga bilioni 9.3 za Burundi (sawa na shilingi bilioni 8.4).
“Kwa utendaji mzuri kama huo, CRDB ilijitokeza kuwa mkopeshaji mwenye faida kubwa zaidi nchini Burundi,” alisema Siwale, akihusisha mafanikio hayo na mbinu za kiubunifu za uendeshaji.
Mkopeshaji huyo, ambaye amekuwa akifanya kazi nchini Burundi kwa miaka 11 iliyopita, kupitia ubunifu, alifanikiwa kuongeza idadi ya mawakala wa benki (wakala) hadi 1,500 kote nchini kutoka 630 mwaka jana.