The House of Favourite Newspapers

Dakika 120 Za Mcongo Simba Acha Kabisa

KWA mara ya kwanza baada ya kutua nchini na kujiunga na kikosi cha Simba, kiungo mpya wa timu hiyo, Kakule Mighuen Fabrice raia wa DR Congo, juzi Jumatatu alianza mazoezi kwenye timu hiyo na kuonyesha uwezo mkubwa huku mashabiki wao wakiwapiga vijembe wa­tani wao Yanga kuwa wata­pata tabu sana msimu ujao.

 

Kiungo huyo, alianza mazoezi ya timu hiyo juzi Jumatatu jioni baada ya kutua nchini kwa ajili ya kusaini mkataba wa kuichezea Simba baada ya kaimu kocha mkuu wa timu hiyo Mrundi, Masoud Djuma kumpendekeza katika usajili wake.

 

Fabrice wakati wowote atasaini mkataba kama wakifikia muafaka mzuri na muwekezaji wa timu hiyo, Mohammed Dewji ‘Mo’.

 

Katika mazoezi hayo yaliyo­fanyika kwenye Uwanja wa Boko Beach Veterani jijini Dar es Sa­laam, Fabrice anayecheza nafasi ya kiungo namba 6 na 8 alionye­sha kiwango cha hali ya juu ka­tika upigaji wa pasi, kukontroo na kukokota mpira na kutengeneza nafasi za mabao huku akipiga pasi za visigino hali iliyosaba­bisha mashabiki waliojitokeza mazoezini hapo wamshangilie na kumpigia makofi kwa kumsifia.

 

Kiungo huyo ambaye ujio wake uliripotiwa kwa mara ya kwanza na Championi akitokea klabu ya Kiyovu Sports ya Rwanda alionyesha makali yake baada ya kocha Djuma kumtaka kuanza mazoezi kwa saa mbili sawa na dakika 120, huku akisubiria kusaini mkataba.

 

Akiwa uwanjani hapo Mcongo huyo ambaye ujio wake ume­fanywa na kocha wa timu hiyo, Masoud Djuma alionyesha uw­ezo kwenye kupiga pasi ambapo wakati mazoezi yanaanza hadi yanamalizika alipiga pasi 32 na tano pekee ndiyo alipoteza huku 27 zikiwafikia wenzake na yeye akifanikiwa kupokonya pasi mbili za wapinzani.

 

Mcongo huyo hakuishia hapo kwani alizidi kuonyesha yupo vizuri baada ya kutengeneza nafasi nne za mabao na akipiga mashuti matatu hali iliyoonyesha kuwakosha mashabiki wengi wal­iojitokeza katika mazoezi hayo. Kiungo huyo hakuishia hapo kwani alionyesha yumo kwa kuonyesha makeke ya kuwapiga tobo na kanzu wapinzani wake pamoja na kutumia msuli pale ambapo alienda kupambania mpira.

 

Kila zoezi ambalo lilikuwa lina­tolewa na kocha Djuma, kiungo huyo alifanya kwa kiwango cha juu ikiwemo kukimbia kwa spidi, mazoezi ya viungo pamoja na mechi ya muda mfupi ambayo ilivigawa vikosi viwili. Kikosi chake kiliundwa na Moses Kitan­du, Abdul Suleiman, Mohamed Rashid, Mohammed Ibrahim na yeye Fabrice.

 

Mara baada ya kumalizika kwa mazoezi hayo, Djuma maarufu kama Irambona, alimuelezea kiungo huyo ambapo alisema: “Kiungo huyo kwa sasa yupo kwenye mazungumzo na uon­gozi wa Simba na kama akifani­kiwa kukubaliana na viongozi wa Simba atasaini mkataba wa kuanza kuitumikia timu yetu.”

 

“Kitu ambacho kitakachom­zuia Fabrice asisaini Simba lab­da afeli kwenye vipimo atakavy­ofanyiwa kabla ya kusaini, lakini kuhusu kiwango mimi kama kocha sina shida naye kwani ni mchezaji niliyewahi kukaa naye nikimfundisha kwa kipindi cha miaka mitatu,”alisema Djuma ambaye mashabiki wa Simba wametokea kumkubali zaidi.

Comments are closed.