The House of Favourite Newspapers

THE DARKEST HOURS (SAA ZA GIZA TOTORO)- 3

ILIPOISHIA:

“Inuka na ufanye ninachokueleza, ukizingua unajua nini kitatokea,” nilisema kwa sauti ya chini lakini yenye mamlaka, yule mwanamke akakurupuka akiwa ni kama haamini kilichotokea, Suma naye akawa anatetemeka akiwa haelewi nimeingiaje pale.

SASA ENDELEA…

“Snox! Nakuomba mdogo wangu, please show me some mercy!” (Nionee huruma tafadhali) alisema Suma huku akiwa anatetemeka kuliko kawaida lakini sikumjali.

“Look at my face!” (Nitazame usoni), nilimwambia kwa Kiingereza kilichonyooka, akanitazama usoni halafu akawa ni kama ameshtuka kidogo.

“Mlikuja mkanipiga na kunijeruhi kiasi hiki, mkamteka Saima wangu na kama hiyo haitoshi, mmekuja kuchoma moto nyumba yetu. Bado unategemea kwamba nitakuonea huruma?” nilisema huku na mimi nikitetemeka kwa hasira.

”No! Nisikilize kwanza Snox,” alisema huku akiniita kwa jina langu la kazi. Watu wengi mitaani huwa wanaamini Snox ni jina langu halisi kwa sababu kila ninakoenda ndilo linalotumika lakini ukweli ni kwamba halikuwa jina langu halisi wala halikuwa na uhusiano wowote na jina langu halisi.

Kiuhalisia jina langu naitwa Keneth au Kenny lakini kama nilivyosema, waliokuwa wakinijua kwa jina hilo, walikuwa wachache mno, tena wale wanaonijua tangu nikiwa mdogo lakini wengine wote walikuwa wakiniita Snox.

“Najua mlitumwa, nataka kujua mhusika ni nani,” nilisema huku nikimkokota taratibu kuelekea kule uani. Yaani ungeshuhudia kilichokuwa kinaendelea, pengine ungepata picha halisi ya kile wanachosema ‘sungura kamkaba tembo’.

Suma alikuwa na mwili mkubwa uliojengeka kimazoezi lakini licha ya ukweli kwamba mimi nilikuwa na kamwili kadogo ka wastani, nilikuwa namkokota kama ng’ombe anayepelekwa machinjioni.

Kwa jinsi nilivyoingia eneo lile mpaka kumpata, bado alikuwa amepigwa na butwaa na hiyo pekee ilitosha kumchanganya kichwa na kibaya alikuwa anafahamu akili zangu nikishika ‘mashine’ zinakuwaje kwani tumewahi kufanya ‘kazi’ pamoja.

“Nataka jibu, sitaki blaah! Blaah!” nilisema huku nikizidi kulikandamiza bomba la AK47 kwenye ubavu wake, nikaikoki na kumfanya ashtuke.

“Nitakwambia Snox, mimi na wewe tumeshakuwa kama ndugu, huna haja ya kutumia nguvu kwangu,” alisema Suma kwa upole, nikatega masikio kwa makini kumsikiliza.

“Mzee anasema umemsaliti, anataka kuhakikisha unapata taabu mpaka mwenyewe ukome.”

“Mzee gani?”

“Aah Snox, kwani nikisema mzee wewe unaelewaje? Kuna mwingine tena zaidi ya bosi?”

“Nimemsaliti kivipi?”

“Kitendo cha kukataa kazi bila sababu za msingi, kimemkasirisha sana na anasema atahakikisha anakomaa na wewe mpaka aone mwisho wako,” alisema Suma lakini maneno yake hayakuniingia akilini. Nilijua kabisa kwamba ananidanganya kwa sababu alichokisema hakikuwa na uzito wowote wa kumfanya mtu aniwinde kwa kiasi kile.

“Saima yuko wapi?”

“Sijui chochote kuhusu Saima, sikuhusika kwenye hiyo kazi.”

“Unanificha si ndiyo?”

“Snox, sina sababu ya kukuficha chochote ndugu yangu, ila labda Seba anaweza kuwa anajua chochote maana siku hizi ndiyo mtu wa karibu zaidi na mzee.”

“Nitampata wapi?”

“Lazima muda huu atakuwa anakula bata Trace Element, kule Masaki,” alisema Suma akitegemea kwamba baada ya maelezo hayo nitamuachia.

Kwa walichonifanyia, japokuwa sikuwa na nia ya kukatisha maisha ya mtu yeyote, lakini ilikuwa ni lazima niwashikishe adabu wote waliohusika halafu mwisho nitamalizia na huyo aliyewatuma, ambaye nilikuwa na hasira kali sana juu yake kwa alichonifanyia maishani mwangu.

Nilimsukuma Suma kwa nguvu, akakimbia na kusimama mbele hatua kadhaa mbele, akanigeukia haraka huku akiwa ameinua mikono juu maana alikuwa anajua ni nini ninachotaka kukifanya. Mara nyingi kama mtu amekuteka na mkononi ana silaha ya moto, anapokwambia ukimbie, au anapokusukumia mbali na yeye, usidhani anafanya hivyo kwa sababu kweli amekusamehe, mara nyingi ni kwa sabahu anataka apate nafasi ya kukulenga vizuri ili akupige risasi. Suma alilijua hilo na ndiyo maana alifikia hata hatua ya kunipigia magoti akiomba nisimfanyie chochote.

Sikutaka kusikiliza la muadhini wala mchota maji, nilifanya kile nilichoona kinafaa, mlio mkali wa bunduki ulisikika, na hasa ukizingatia kwamba ilikuwa imekatwa mtutu, mlio wake ulikuwa mkubwa na wa kutisha sana.

Sikupoteza muda, nilimruka pale chini alipokuwa ameangukia akitokwa na damu nyingi, nikachumpa kwenye ukuta na muda mfupi baadaye, nilikuwa nikiteremka upande wa pili wa ukuta. Nilijua kwa vyovyote lazima mlio huo urtasikika kwa polisi waliokuwa doria ambao lazima watakuja eneo hilo kwa hiyo nilipita njia tofauti na niliyojia.

Wateja waliokuwa wakiendelea kuburudika mle ndani kwa vinywaji na muziki, walishtuka mno kusikia mlio wa bunduki, tena kutokea ndani kabisa ya ‘chimbo’ lao, kila mmoja akaanza kutimua mbio kuokoa maisha yake, wengine wakikanyagana hovyo na kusababisha madhara yawe makubwa.

Zile purukushani zilinisaidia hata mimi kuondoka eneo hilo kwa urahisi zaidi kwani nilijichanganya na kujifanya na mimi naogopa mlio wa risasi, nikawa nakimbia ‘mdogo-mdogo’. Ungeniona wala usingeweza kuhisi kwamba mimi ndiyo nilikuwa chanzo cha mshike-mshike uliokuwa unaendelea.

Nilitokezea Sinza ya Mugabe baada ya kuwa nimekatiza sana vichochoro ili nisionekane na mtu yeyote. Nilisimama kando ya barabara na muda mfupi baadaye, bodaboda moja ilikuja, nikaipungia mkono na hatimaye ikasimama.

‘Duh, baba umepiga pigo za kijambazi kabisa! Niuzie hilo koti,” alisema dereva wa bodaboda huku akichekacheka, nikanyamaza tu kwani ninapokuwa nimeivaa sura ya kazi huwa sipendi kucheka kwa sababu nimewahi kufundishwa kwamba unapocheka, unaondoa uzingativu wa akili.

“Nipeleke Trace Element.”

“Trace Element au Element?”

“Nimekwambia Trace Element,” nilisema kwa msisitizo, yule dereva wa bodaboda akanywea na nikamuona kama ananitazama kwa macho ya kuibia hivi. Basi aliwasha pikipiki na tukaondoka huku kila mtu akiwa kimya kabisa. Njia nzima nilikuwa namsisitiza kuongeza kasi nadhani mpaka mwenyewe baadaye alikoma.

Basi baada ya kama dakika thelathini, tayari tulikuwa tumewasili Masaki, nikateremka kwenye bodaboda na kumlipa fedha zake kisha harakaharaka nikajichanganya na kuelekea kwenye chimbo lingine liitwalo Trace Element.

Unajua watu wengi wanapajua Club Element lakini hawajui kwamba kuna chimbo lingine la kijanja liitwalo Trace Element, ambalo ndani yake kuna watu wabaya wa kila aina.

Mara nyingi, wau wabaya huwa hawachangamani na watu wazuri mara kwa mara, hata wanapokunywa pombe, huwa wanatenga kujificha kwenye machimbo yao ambayo wanakutana wenyewe kwa wenyewe, hapo ndipo wanapokuwa na amani ndani ya mioyo yao kwani wakijichanganya na watu wasiowajua, kila anayemuona anahisi ni polisi au mpelelezi.

Kwa sababu mara kwa mara nilikuwa nakuja eneo hilo na wenzangu wakati nikiwa mwanachama kamili, nilikuwa nazijua njia nyepesi za kutoroka, hasa polisi wanapokuja kwa lengo al kufanya ukaguzi, niliamua kutumia njia hizohizo kuingilia kwa sababu nilikuwana uhakika pale getini nisingeruhusiwa kuingia.

Basi nilizunguka upande wa pili na kukwea juu ya mti uliokuwa jirani na fensi, nikatambaa na kujivuta juu kwa juu mpaka nilipopanda juu kabisa ya fensi, nikatafuta sehemu nzuri ya kurukia, nikadondokea ndani kimyakimya bila mtu yeyote kujua.

Unaweza kushangaa huu umahiri wa kuparamia kuta za watu, taha ndefu kiasi gani bila kushtukiwa na mtu yeyote nimeupata wapi? Katika kipindi chote nilichokuwa nafanya kazi za uhalifu, mimi ndiyo nilikuwa nategemewa zaidi kwenye masuala ya kuruka fensi na kwenda kufungua mageti kwa ndani.

Mara nyingi ili majambazi waingie ndani kwa urahisi, lazima mmoja atangulie ndani kupitia ukuta na akiingia, anaenda kufungua geti kwa ndani ili wote waliopo nje waingie na huko ndiko nilikopata ujuzi huo.

“Kumbe wakati napanda kwenye ule mti, mmoja kati ya walinzi wa eneo hilo, alikuwa ameshaniona na akawa anasubiri aone mwisho wangu. Nikiwa pale chini, nilishtukia bomba la baridi likinigusa shingoni, likifuatiwa na sauti ya ‘tulia hivyohivyo kwa usalama wako)’, nikajua nimepatikana.

Je, nini kitafuatia? Usikose Ijumaa kwenye Gazeti la Championi Ijumaa au bofya  Simulizi za Majonzi kusoma mwendelezo.

Comments are closed.