Diamond ‘Awashinda’ Wanaharakati Mitandaoni
MITANDAO hii ya kijamii sasa hivi ni hatari sana. Watu wanaweza kuamua kueneza uvumi wa jambo fulani na likaungwa mkono na watu wengi hadi likaonekana kama ni la maana kumbe halina maana yoyote.
Wabongo wako bize sana na mawazo hasi kuliko mawazo chanya. Yani mtu anakuwa hodari wa kusambaza sana taarifa hasi za mtu fulani kuliko taarifa chanya za mtu huyo huyo. Nadhani wanapenda sana watu wafikwe na mabaya.
Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ alipotajwa kuwania tuzo za BET, wapo watu wanaojiita wanaharakati walijenga hoja zao mitandaoni ili tu Diamond aonekane ni mtu hasi katika jamii hivyo hastahili kuungwa mkono katika jambo hilo.
Yaani kampeni ilindeshwa kwamba Diamond ni mtu ambaye alikuwa anasapoti Chama Tawala kwenye uchaguzi Mkuu uliopita na hakuwahi kusapoti mambo ya vyama vingine.
Wakaenda mbele zaidi kwa kusema, hajawahi kukemea mambo mabaya yaliyokuwa yanafanywa na chama tawala pamoja na Serikali kwa ujumla. Wakasema alikuwa kimya wakati vifo mbalibali vilipokuwa vinatokea.
Hakusimama mstari wa mbele kueleza uovu iliokuwa unafanyika katika jamii hivyo hana sifa ya kuwa msanii. Propaganda hiyo ikaenda mbali hadi kuchapisha maandiko kwenye tofau balimbali kueleza kuwa Diamond ameshiriki kwenye uovu hivyo hastahili kuwa BET.
Hayo yote yalifanywa kwa mara ya kwanza na wanaharakati ili kuwashawishi hata wale waandaaji wa tuzo hizo waweze kumtoa Diamond.
Bahati mbaya sana uwezo wa watu wengi kuchuja mambo kwenye mitandao ni mdogo sana.Matokeo yake, walikuwa wanayabeba tu mambo hayo na kuyasambaza kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii.
Watu wa kuunga mkono harakati hizo wakawa wengi tu. Bila kujua kwamba waandaaji wa tuzo hizo, hawapokei kura kutoka kwa mashabiki lakini watu hao walikomaa na kampeni ya kusema Diamond asipigiwe kura.
Kampeni ikawa ni kuwaeleza watu kwamba Diamond hastahili kupigiwa kura.Watu kama kina Mwijaku wakawa wengi. Kwa kujua au kutokua Mwijaku anatumika na nani, watu wengi waliingia mkenge tu kumpinga Diamond. Lakini yote hayo yalikuwa yakiendehswa ili staa huyo anayesumbua na wimbo wa Kamata, aondolewe kwenye kinyang’anyiro hicho.
Mungu siku zote sio Athuman, Diamond hakuondolewa na jina lake likaendelea kuwepo kwenye mtandao wa BET mpaka siku ya mwisho ya kumtangaza mshindi Juni 27 mwaka huu.
Hili ndugu zangu ni tatizo na tunapaswa kama taifa kujitathimini.Kweli tuna nia ya dhati ya kuishi kama Watanzania au tunataka kuendelea kuishi kwa matabaka? Matabaka haya yatatusaidia au yanazidi kutubomoa. Unajaribu kuangalia wanaharakati hao ni watu ambao wanafahamika na wana heshima kubwa katika jamii, wanatufundisha nini?
Tunatakiwa kuchuja haya mambo kwa akili zetu kabla ya kusambaza habari za hawa wanaharakati. Chuki binafsi za mtu na mtu zisitugawe sisi wengine ambao tunafuatilia muziki mzuri. Unapomuingiza Diamond kwenye mambo ya siasa, si sawa.Kila mtu ana uhuru wa kuchagua chama cha siasa hivyo kitendo cha mtu kuwa chama fulani haimaanishi kwamba yeye ni adui.
Ni sawa sawa na mpira wa miguu au dini, kila mtu ana uhuru wa kuchagua dini au timu ya kuishabikia.Unapomuona mtu anashabikia upande fulani, asichukuliwe kama ni adui.
Kila mtu ana uhuru wake. Wasanii wao kazi yao ni kuelimisha, kuburudisha na mambo mengine. Haya mambo ya kuwalazimisha wafanye kazi za kisiasa ni kuwakosea.Bahati mbaya sana linapokuja suala la siasa, nao unaweza kuwakuta wana mtazamo wao hivyo inakuwa vigumu kukubaliana nao.
Hebu angalia sasa hivi wanaharakati wanamuangaliaje Diamond ambaye hakutolewa kwenye tuzo hadi dakika za mwisho?Muziki mzuri siku zote ndio unaoweza kukupa mafanikio.
Kuna namna ya kujitangaza na fitna za gemu, waambieni na wasanii wengine ambao mnatamani wamzidi Diamond wajipange ili na wao wawe wakubwa.Ndio maana wengi wamekalia majungu, wamekuwa wakimsema kila siku Diamond halafu mwenzao anakimbia tu yani anaupiga mwingi na mafanikio yanaonekana, wanaharakati tubadilike.
MAKALA: Mwandishi Wetu Mwandishi Wetu | Risasi Jumatano