The House of Favourite Newspapers

Diamond Mfalme Mpya Afrika

HUYU ndiye mfalme mpya Afrika! Hizo ndizo kauli za watu wengi walioitazama shoo ya mtoto wa Tandale, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ huko Dubai katika Falme za Kiarabu, Gazeti la Ijumaa Wikienda limekukusanyia stori nzima.

 

Mchongo mzima ulichukua nafasi usiku wa kuamkia juzi, kwenye shoo iliyowakusanya wasanii wengi wakubwa kutoka barani Afrika iliyofahamika kwa jina la One Music Africa Fest.

 

BALAA ZITO LIMEMBEBA

Ufalme huu hakupewa tu kirahisi, balaa zito alilolifanya mkali huyo ndilo lililombatiza ufalme huo ambao awali ulikuwa ukishikiliwa na wasanii kutoka Nigeria wakiwemo kina David Adedeji Adeleke ‘Davido’, Damini Ebunoluwa Ogulu ‘Burna Boy’, Augustine Miles Kelechi ‘Tekno’ na Tiwatope Savage ‘Tiwa Savage’.

Awali, ilikuwa ikiaminika kuwa mastaa hao wa Nigeria ndiyo ambao walikuwa wakiheshimika zaidi Afrika ambapo mitandao mbalimbali ya kiburudani kwa nyakati tofauti imekuwa ikitoa tathmini kuonesha wanaongoza, kuna nyakati aliongoza Davido na hivi karibuni, Ayodeji Ibrahim Balogun ‘Wizkid’ ndiye anayetajwa kuwa wa moto zaidi.

TWENZETU DUBAI KIMAANDISHI

Siku hiyo, walipanda baadhi ya wasanii hao wanaotokea Nigeria na kufanya makamuzi yao ya kawaida, lakini ilipofika zamu ya Simba au Mondi, hali ya hewa ilichafuka kwa shangwe si la nchi hii.

MC wa shughuli hiyo, alianza kumpamba Diamond kwa maneno ambayo yalitengeneza ‘awareness’ kubwa kwa mamia ya mashabiki waliokusanyika katika mji maarufu wa kiburudani za kitajiri, Dubai Festival City.

“The next performer is coming in the stage…every time this guy heats the stage like electricity, its fire, its performance is another level, we came from Nigeria we go to Tanzania right now, ladies and gentleman look at your chain, look at your jewellery if you wanted to be Diamond, if you wanted to be Platnumz.

“Are you ready? Ladies and gentleman are you ready? Make some noise for the incredible, the one and only Diamond Platnumz lets goooo…Diamond Platnumz lets gooooo,” aliamsha popo MC huyo akiwa ameshamwagia sifa kama zote kwamba Mondi anapokuwa jukwaani ni habari nyingine.

Alimaanisha kwamba ni moto kwelikweli, analiunguza jukwaa na ni levo nyingine ukilinganisha na amshaamsha iliyotoka kufanywa na wasanii wa Nigeria, hivyo yaani!

SHOO YA KIBABE

Baada tu ya kumwagiwa sifa hizo na shangwe likiwa limetawala, Diamond aliingia jukwaani na kuanza kukinukisha ambapo alianza na Wimbo wa Yope alioshirikishwa na Mkongomani Innocent Didace Balume ‘Innoss’B’.

Shoo ikachanganya na shangwe likawa si la kitoto kutoka kwa mashabiki ambapo aliimba nyimbo zake kibao maarufu ikiwemo Tetema na Live You Die alioshirikishwa na mkali kutoka Nigeria, Patrick Nnaemeka Okorie ‘Patoranking’.

KILICHOMBEBA ZAIDI

Kwenye shoo hiyo, Diamond alionekana kueleweka zaidi kwa mashabiki kwani waliimba naye mwanzo mwisho nyimbo zake na mara kadhaa DJ alikuwa akizima muziki na kuwaacha mashabiki waimbe wenyewe kisha kurudisha kidogo na kuuzima tena.

Baada ya shoo hiyo kuisha, mitandao mbalimbali ya kiburudani ya Dubai na nje ya jiji hilo la maraha, ilionesha kuguswa zaidi na shoo ya Diamond. Kuna ambayo ilidai, Diamond ameshaufunika ufalme wa Wizkid, lakini baadhi ilisema, anashika nafasi ya pili baada ya Wizkid.

TATHIMINI YA WIKIENDA

Tathmini ya jumla ambayo iliyofanywa na Gazeti la Ijumaa Wikienda, ilidhihirisha kweli Mondi ni mfalme mpya wa muziki wa Afrika kutokana na mitandao mingi kumbeba.

ORODHA KAMILI YA MASTAA WALIOKAMUA

Orodha kamili ya mastaa wa Afrika waliopiga shoo hiyo ni; Davido, Wizkid, Burna Boy, Teni, Tekno, Tiwa Savage, 2 Baba, Zlatan, Jah Prayzah, Akothee, Betty G, Lij Micheal, Linah, Kcee, Mondi, Harmo, Eddy Kenzo, Nandy na Nhatty Man. Wengine ni Souhila, The Ben, Vanessa Mdee, King Promise, DJ Spinall, DJ Cuppy, DJ Ob na DJ Xclusive.

 STORI: ERICK EVARIST, DAR

Comments are closed.