ALLY Mohamed ambaye ni meneja wa winga wa Dodoma Jiji FC, Dickson Ambundo, amefunguka kuwa mteja wake huyo atakuwa mchezaji rasmi wa Yanga siku za hivi karibuni kwa kuwa kila kitu kinaelekea kukamilika.
Meneja huyo alisema walishapokea ofa kutoka Yanga na wameshafikia kwenye asilimia zaidi ya 90 ili mchezaji huyo kusaini dili hilo, hivyo hakuna namna ambayo inaweza kushindikana.
Akizungumza na Spoti Xtra, Ally alisema: “Yanga tumeshafika nao katika hatua nzuri ya kukamilisha hili dili, kwa sababu waliwasilisha ofa na tukawa tumefikia kwenye hatua nzuri sana na ndiyo maana naweza kusema mambo yapo vizuri kabisa na hakuna shida.”Spoti Xtra lilimtafuta Ambundo ili kujua kuhusu yeye, ambapo alisema:
“Kiukweli kila kitu nimemuachia meneja na uongozi wangu uweze kusimamia kila kitu, kazi yangu mimi ni kucheza soka na siyo kitu kingine.”
Taarifa kutoka Kambi ya Dodoma Jiji zimeeleza kuwa, Ambundo amegoma kuongeza mkataba na ameshawaaga wenzake kuwa anatimkia zake Yanga msimu ujao.Soma Uk 16 makala ya Dickson Ambundo akifunguka mengi kuhusu maisha yake na ishu ya kutua Yanga.
STORI: ISSA LIPONDA, Dar es Salaam