Dkt. Kairuki Awapa Somo la Uzazi, Ujauzito na Ugumba Wamama wa Goba
DAKTARI Bingwa wa Kinamama, Wajawazito na Bingwa wa tatizo la Ugumba, Clementina Kairuki ambaye ni Mkurugenzi wa Hospitali ya Kairuki iliyopo Mikocheni jijini Dar, amewapa somo la uzazi, ujauzito na Ugumba Wamama wa Goba katika tamasha lao la ujasiriamali wanalofanya kila mwaka.
Akizungumza na wamama hao, Dkt. Kairuki alizungumzia tatizo la uzazi, ujauzito na ugumba na kueleza jinsi linavyopelekea ndoa nyingi kuvunjika kutokana na wanandoa wengi kukosa uelewa.
Amesema tatizo la ugumba au kuchelewa kushika mimba mara nyingi linasababishwa na kuziba kwa mirija ya uzazi na sababu nyingine kadhaa ikiwemo kuharibu mimba mara kwa mara na kutumia dawa za kuzuia mimba bila ushauri wa kitaalamu.
Dkt. Kairuki amesema tatizo la uzazi la katika familia haliwahusu wanawake peke yao na kusema hata wababa nao wapo wanaokabiliwa na tatizo hilo ingawa wamekuwa wagumu kujikubali, alisema Dkt. Kairuki.
“Kwa yeyote anayejihisi kuwa na tatizo hilo namshauri afike kwenye vituo vya afya na kuwaona wataalamu kwa ajili ya tiba na ushauri kwakuwa tatizo hilo linaweza kumalizwa na wataalamu na sio kukimbilia kuvunja ndoa”. Alimaliza kusema Dkt. Kairuki.
HABARI/PICHA: RICHARD BUKOS /GPL