WAKATI Bahati Nasibu ya Shinda Nyumba Awamu ya Pili ikiendelea katika hatua ya droo ndogo, ambapo wiki iliyopita ilichezeshwa ya nne, mshindi wa zawadi kubwa, Shabani Ahmadi Ngao ambaye ni mkazi wa Tabata jijini Dar es Salaam, ametoa kauli ya kusisimua.
Ngao ambaye ni msomaji wa muda mrefu wa magazeti ya Global Publishers ambayo ni Ijumaa, Championi, Risasi, Amani, Uwazi na Ijumaa Wikienda, siku zote hakuwahi kufikiri kama anaweza kupata ushindi kwa kujaza kuponi za bahati nasibu ya shinda nyumba, ingawa tangu ianze anafahamu uwepo wake.
“Mimi nilikuwa nikinunua gazeti nasoma vitu ninavyovihitaji halafu naliacha naendelea na mambo yangu, sasa siku moja kumbe mke wangu naye alikuwa akiyasoma na akagundua kuwa nilikuwa sikati wala kujaza kuponi za shinda nyumba, akaniambia hata kama nadhani sitashinda lakini angalau nijaze tu kuliko kuziacha kuponi zipotee.
“Kwa kweli sikudhani kama naweza kushinda maana haya mambo bwana wakati mwingine mtu unashindwa kuamini, basi nikaanza kujaza kuponi, sasa siku napigiwa simu kuwa nimeshinda, ikabidi nimtaarifu mke wangu ambaye alifurahi sana,” anasema Ngao.
Kuonyesha kuwa mkewe alikuwa na mchango mkubwa katika ushindi wa pikipiki aliyopewa kwa kuibuka mshindi wa zawadi kubwa katika droo ndogo ya nne, Ngao alifika katika hafla ya kukabidhiwa kifaa hicho cha moto akiwa ameongozana na mkewe, Leyla Alex.
“Mimi ni msomaji mzuri wa magazeti ya Global kwa kipindi kirefu, lakini awali nilikuwa nasoma bila kujaza kuponi lakini huyu mke wangu ndiye aliyenihamasisha kukata kuponi na kushiriki mchezo huu.
“Ndiyo maana hata leo nikaona nisimuache nyumbani, bora nije naye ajionee mwenyewe jambo jema alilonishauri na kutimia, Mungu ambariki sana mke wangu Leyla,” alisema Ngao ambaye baada ya kupewa zawadi yake, aliiwasha na kuondoka nayo akiwa amempakiza mkewe.
Licha ya Ngao, washindi wengine saba waliibuka na zawadi mbalimbali ikiwa ni pamoja na simu za kisasa aina ya Phantom 6, dinner set na watu wengine watano ambao walijishindia zawadi ya ving’amuzi kutoka Kampuni ya Ting.
Afisa Masoko wa Global Publishers Yohana Mkanda, aliyekuwepo katika hafla hiyo ya kuwakabidhi washindi zawadi aliendelea kusisitiza juu ya wasomaji kuendelea kukata kuponi kwenye magazeti hayo, wakati huu bahati nasibu hiyo ikielekea kunoga zaidi.
“Kwenye magazeti yetu yote, katika kurasa za pili zipo kuponi zenye maelekezo ya namna ya kufanya, ukishamaliza kujaza, unaweza kuzituma kwetu kupitia kwa mawakala wetu waliopo nchi nzima au wale wa Dar es Salaam wanaweza kuja ofisini kwetu, Bamaga Mwenge na kuziacha kwenye ndoo ya kukusanyia kuponi,” alisema Mkanda.
Bahati Nasibu hii Shinda Nyumba Awamu ya Pili imedhaminiwa na Kampuni ya Tecno Mobile, King’amuzi cha Ting, British School na Kilimanjaro Institute of Technology.
MAKALA: RICHARD BUKOS IJUMAA WIKIENDA