Eng. Hersi Auchambua Utamu wa YangaSC
MKURUGENZI wa Uwekezaji wa GSM na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili Yanga, Eng Hersi Said amesema kuwa Yanga ambayo ilicheza mbele ya Simba ndiyo timu ambayo wanahitaji kuwa nayo hadi mwisho wa msimu.
Hersi aliichambua Yanga kwa kusema kuwa, timu hiyo imekuwa tamu kwenye kila idara, kwa sababu kuanzia kipa hadi mshambuliaji wa mwisho wote wanacheza kwa daraja la juu.
Hersi aliliambia Championi Jumatatu kuwa, Yanga hii itafanya makubwa zaidi kwenye soka la Bongo msimu huu, ingawa ilikuwa bahati mbaya kwao kuondoshwa mapema kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika. “Hii ndiyo timu ambayo Wanayanga walikuwa wanaitaka, timu inacheza kuanzia nyuma hadi mbele kwa mshambuliaji kule, ukitazama wanaocheza ndani wote bora.
“Ukigeuka kwenye benchi kwa wachezaji wa akiba nako kuna wachezaji bora, huo ndiyo utamu wa Yanga ya msimu. Niombe mashabiki waendelee kuisapoti Yanga yao,” alisema Hersi.
ISSA LIPONDA, Dar es Salaam