The House of Favourite Newspapers

EPUKA HILI UNAPOKUWA NA HASIRA NA MWENZA WAKO

JUMAMOSI nyingine Mungu amenijalia afya njema. Tunakutana tena kwenye uwanja wa mahaba, kupeana mambo mbalimbali yanayoweza kutusaidia katika mahusiano. Kizazi cha sasa kimekuwa na matatizo mengi sana katika masuala ya mahusiano. Hii yote inatokana na wengi wetu hatuna misingi mizuri ya kuishi na wenza wetu.

 

Tunaishi kwa mazoea, tunawachukulia poapoa wenza wetu na matokeo yake mambo yanaharibika. Mwenza wako anapoona unamchukulia poapoa, unamdharau kamwe hawezi kufurahia. Lazima mtakasirikiana, mtatukanana na hata kupigana.

 

Ni muhimu sana wapendanao kuwa na mipaka ya kimazungumzo. Kujielewa kwamba unazungumza na mwenza wako utumie lugha gani. Sio unazungumza na mwenza wako kama vile unazungumza na marafi ki zako, jaribu kubadilika kidogo.

 

Kuwa na heshima na mwenza wako sababu huyo ndio mtakayetengeneza ‘taasisi’ yenu ya muda mrefu. Unaachaje kumheshimu mwenza wako ambaye ndiye unayelala naye, ndiye ambaye una mipango naye na ndiye mtakayekuwa pamoja kwa miaka mingi zaidi pengine kuliko hata wazazi wako.

 

Huyo ndiye msiri wako wa maisha. Nazungumza hili kwa sababu kwa kawaida mara nyingi huwa wapendanao wanakutana ukubwani, kila mtu anakuwa ametoka kwenye misingi yake.

Kila mmoja anakuwa amelelewa katika malezi tofauti hivyo msipokuwa makini kusomana tabia, hakika hamuwezi kufi ka mbaliYawezekana mwenza wako akawa na tabia fulani ambayo si nzuri lakini kwa kuwa ndio umemchagua, unapaswa kumuongoza taratibu ili aweze kubadilika. Vaa uhusika wa mpenzi, maanisha kweli huyo uliyenaye ni mpenzi wako.

 

Wengi wetu huwa tunakosea sana kuishi na wapenzi wetu kutokana na kushindwa kuwasoma ni watu wa aina gani hususan pale inapotokea mmekwazana. Pale inapotokea mmepishana kauli, kuna vitu wote wawili mnapaswa kufanya. Kila mmoja anapaswa kujua inapotokea mmekwazana, silaha ya mafanikio yenu iwe kujishusha. Kujishusha kuna faida.

Hili mlifanye wote wawili. Lifanyeni kama vile ndio kauli mbiu yenu pale mnapoona kuna shida. Jengeni iwe kama ndio utamaduni wenu. Msitoe nafasi kutawaliwa na hasira. Kweli mnaweza kubishana lakini kubishana kwenu kuwe kwa masikilizano huku akili yenu yote ikiwaza kitu kimoja tu, kujishusha. Mathalan mwanamke unaweza kuwa wa kwanza kufanya hivyo, kwa kufanya hivyo hata mwanaume hawezi kuwa na ujasiri wa kupanda tena. Atapandaje wakati wewe umepoa? Atapanda pale tu wewe utakapokuwa unataka kubishana naye kwa kumpandia.

Hata kwa wanaume, mnapaswa pia kuwa na utamaduni wakuwasikiliza wanawake wenu. Anapokuwa amepanda ana hasira, msikilize halafu kwa lugha ya kawaida kabisa wewe mueleze kwamba hauoni sababu ya kuendelea na hasira na badala yake unahitaji amani na furaha. Kauli mbiu hiyo ya kuitafuta amani na furaha ikiwa ni sehemu ya maisha yenu, mtaishi vizuri sana.

Kila linapotokea jambo la kuwafanya mgombane, kila mmoja taa ya suluhu imuwakie. Taa ya kudumisha upendo wenu iwe silaha ya kuamua ugomvi wenu. Kila mmoja atambue kwamba maamuzi yanayotokana na hasira siku zote huwa yanakuja kuwa na majuto baadaye. Usipandishe hasira wakati mpo kwenye ugomvi kwani hapo ni rahisi kusema chochote. Akili inaweza kukuongoza uachane na mwenza wako kutokana na usumbufu wa siku moja na kusahau mazuri yote mliyoyajenga kwa miaka mingi. Instagram & Facebook: Erick Evarist Twitter: ENangale.

Comments are closed.