The House of Favourite Newspapers

FAHAMU KINACHOSABABISHA MIGUU KUFA GANZI

 KATIKA mwili wa binadamu, kuna tatizo la kiafya ambalo huambatana na dalili za mtu kuhisi maumivu, kuhisi kuwaka moto na kufa ganzi kwa viungo vya pembezoni mwa mwili yaani kupatwa na ganzi katika misuli ya miguu na mikono.

Tatizo hili kitaalamu hujulikana kwa jina la Peripheral Neuropathy.

Mwili wa binadamu hutawaliwa na mifumo ya neva au kwa kitaalamu Nervous System, ambapo katika mifumo hii kuna mfumo mkuu wa ubongo na uti wa mgongo na pia kuna mfumo wa pembezoni ambao ni kazi za mwili

Mbali na ubongo na uti wa mgongo (peripheral nervous system), mfumo huu wa pembezoni hujumuisha kazi za misuli, mapigo ya moyo, mmeng’enyo wa chakula tumboni, uwezo wa kuhisi baridi/ joto, kugusa vitu na kujua ukali wa ncha ya kitu na kadhalika.

Matatizo haya ya kiafya ya miguu/mikono kuhisi ganzi, baridi au maumivu husababishwa na kuumia au kudhoofika kwa neva za pembezoni mwa mwili yaani miguuni au mikononi na hivyo kupotea kwa uwezo wa kufanya kazi wa neva katika sehemu husika.

DALILI

Dalili zinazoambatana na ugonjwa huu ni hizi zifuatazo: Mtu kuhisi ganzi, maumivu au kuwaka moto maeneo ya miguuni/mikononi, kuhisi kama umevaa soksi au gloves wakati hujavaa, kuhisi kama kuna kitu cha ncha kali kinakuchoma miguuni au kwenye vidole, kushindwa kushika au kunyanyua kitu, kuchoka kwa misuli na kadhalika.

Miongoni mwa mambo ambayo husababisha neva hizi za pembezoni kudhoofika na kushindwa kufanya kazi vizuri ni haya yafuatayo:

Kupungua kwa virutubisho mwilini, katika hili tunamaanisha mwili kutokuwa na vitamini ya kutosha na hasa mkusanyiko wa vitamini B, (Vitamin B Complex), matumizi ya dawa, mtu kuwa katika matumizi ya baadhi ya dawa, mfano dawa za kutibu kifua kikuu au za kupambana na virusi vya ukimwi huweza kumsababishia mtumiaji matatizo ya neva.

Uzito mkubwa wa mwili, hii hupelekea maumbile ya viungo vya mwili mfano umbile la uti wa mgongo lionekane tofauti na ilivyo kawaida, kubadilika huku husababisha baadhi ya neva katika uti wa mgongo zikandamizwe zaidi na misuli/uzito wa mwili na hivyo kusababisha neva hizo zishindwe kufanya kazi vizuri, matokeo yake ni wewe kuanza kuhisi maumivu au kufa ganzi kwa miguu.

Mtu mwenye tatizo la kisukari huwa hatarini zaidi kuugua au kupata matatizo ya neva, (diabetic polyneuropathy).

Mtu kuwa na shinikizo kubwa la damu (High blood pressure) pia ni kihatarishi kinachoweza kumfanya mtu apate ugonjwa huu wa neva.

Baadhi ya vitu hatarishi vinavyoweza kumfanya mtu apate matatizo haya, vinaweza kuepukika kwa mtu kuyabadili maisha yake mfano, kama ulikuwa hufanyi mazoezi ya mwili, basi ujitahidi kuupa mwili mazoezi ili kupunguza uzito wa mwili, kuepuka magonjwa ya kisukari na kuepuka kuwa na shinikizo kubwa la damu.

Pia kula chakula chenye virutubisho vya kutosha na fuata maelekezo ya wataalamu wa afya kuhusu matumizi sahihi ya dawa na kanuni za kukufanya uishi huku ukiwa na afya bora. Matumizi ya dawa kwa muda mrefu hasa za TB na ARV, uzito mkubwa wa mwili husababisha maumbile ya viungo vya mwili mfano umbile la uti wa mgongo huonekana tofauti na ilivyo kawaida.

Kubadilika huku husababisha baadhi ya Neva katika uti wa mgongo zikandamizwe zaidi na misuli/ uzito wa mwili na hivyo kusababisha Neva hizo zishindwe kufanya kazi vizuri, matokeo yake unaanza kuhisi maumivu au miguu/mikono kufa ganzi.

Au kuwa na ugonjwa wa kisukari ama ule wa shinikizo la damu.

MATIBABU NA USHAURI

Jambo rahisi ni kubadili tabia hasa vyakula vinavyochangia tatizo hili. Lakini pia ukiona kila mara unapatwa na ganzi katika misuli ya miguu au mikono muone daktari.

Comments are closed.