The House of Favourite Newspapers

Fanya Haya Kwa Umpendaye Mwezi Huu Mtukufu!

0

NA AZIZ HASHIM | IJUMAA | MAHABA

NAMSHUKURU Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia uzima na kuniwezesha kuiona siku hii ya leo nikiwa salama salimin. Lakini namshukuru pia kwa kuwa amenipa uwezo wa kuandika mada za kimapenzi ambazo zinawagusa walio wengi. Wiki iliyopita nilizungumzia namna ambayo unaweza kujistiri hata kama hujafunga katika mwezi huu mtukufu.
Unakuta mwanamke anajua kabisa kuwa wenzao wapo kwenye mfungo lakini kwa sababu yeye si wa dini hiyo, basi haoni hatari kuvaa kihasara na kutembea hadharani.

Kwa kifupi, uungwana ni vitendo, hebu onesha uungwana wako kwa siku hizi chache tu za Mwezi Mtukufu kisha baada ya hapo ruksa kuendelea na staili yako ya maisha. Baada ya hayo, wiki hii nazungumzia suala la mapenzi hasa katika kipindi hiki ambacho Waislam bado wako katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani. Nimekuwa nikipokea maswali mengi kutoka kwa baadhi ya wasomaji wangu wakiuliza mambo kadhaa kuhusu uhusiano wao.
Wapo ambao ni wapenzi na kipindi hiki inaonekana mahaba yamepungua kutokana na mmoja au wote kuwa katika mfungo. Wapo wanaolalamikia wapenzi wao kutotaka hata kuonana nao kwa maelezo kwamba, wakikutana eti swaumu zitaharibika. Si hivyo tu, wapo wanaosema siku hizi mawasiliano yamekuwa hafifu, hakuna SMS tamu, hakuna kupigiana simu kuzungumza mambo matamu. Katika hili kwanza niseme tu kwamba, kupendana hakuna mipaka.
Kila  dakika, kila saa, kila siku na kila sehemu tunatakiwa kuoneshana mapenzi sisi tulio katika uhusiano wa kawaida lakini pia wale walio katika ndoa. Kikubwa cha kuzingatia ni kutii sheria za kidini zilizopo. Hata hivyo, wiki hii nataka kuzungumzia mambo kadhaa ambayo wapenzi wanatakiwa kuyazingatia hasa kwa kipindi cha mwezi huu mtukufu.  Nimediriki kuzungumzia mada hii kwa kujua kwamba, mapenzi hayachagua dini, wapo waliopendana wakiwa katika dini tofauti, namaanisha Muislam na Mkristo.

Katika mazingira haya ni lazima kutakuwa na matatizo kama mambo kadha wa kadha hayatazingatiwa na hili litakuja kama kila mmoja ataheshimu imani ya mwenzake na kuwa tayari kuvumilia kwa kila jambo. Kukutana, kuongea ruksa! Jamani nani kasema ukiwa umefunga usikutane na mpenzi wako? Kuna tatizo gani kama mtakutana na kubadilisha mawazo kuhusiana na maisha yenu? Kinachokatazwa hapa ni kutegana kimahaba kiasi cha kumfanya mpenzi wako afikie hatua ya kuiharibu swaumu yake.

Cha kuzingatia katika hili ni kuhakikisha humpi mpenzi wako vishawishi, zungumza lugha nzuri na pia mavazi yako yawe ya kujistiri hasa kwa wanawake. Fahamu kama mpenzi wako kafunga au mmefunga wote, ni kipindi cha kutubu dhambi zenu lakini pia kama hamjaoana basi ni wakati wa kumuomba Mungu awajaalie muweze kuoana haraka.
Hata hivyo, katika suala la kukutana, isiwe mara kwa mara. Nasema hivyo kwa kuwa najua sisi ni binadamu, unaweza kukutana na mpenzi wako fikra zako zikakupeleka kusikotakiwa na ukatamani kuonja na utakuwa umefanya kosa kubwa. SMS na kupigiana simu kuwe na mipaka.

Meseji zile za chumbani hazina nafasi kipindi hiki na ukimtumia mpenzi wako SMS za kingono ni matatizo kwako na kwa mwenzako, sasa kwa nini umuingize matatizoni mtu unayempenda? Haya yote si kwa mchana tu, ni kwa saa 24 maana kuna ambao mchana wanafunga, usiku mahaba kama kawa wakati hawajaoana. Waliooana ndiyo walioruhusiwa kufanya mapenzi na tena ni baada ya kufuturu, wao wana haki hiyo. Tukumbuke tu kwamba, zinaa imekatazwa, si kipindi hiki tu bali katika siku zote za maisha. Kwa maana hiyo basi, tujizuie kumkera Mungu lakini pia muombe dua ikiwezekana mwezi huu mtukufu ukiisha, muoane ili muweze kuyafurahia maisha yenu ya kimapenzi. Ni hayo tu kwa leo, tukutane tena wiki ijayo kwa mada nyingine.

Leave A Reply