The House of Favourite Newspapers

 FAYMA AFUNGUKIA NDOA YAKE NA RAYVANNY

NI mrembo hasa lakini sifa kubwa ambayo inamfanya aendelee kuonekana mrembo kila kukicha ni heshima na upendo wa dhati alionao kwa watu hususan mashabiki wake, mara kadhaa baba wa mtoto wake msanii wa Bongo Fleva, Raymond Mwakyusa ‘Rayvanny’ amekuwa akinukuliwa akimsifia mwanamke wake huyo kuwa ni mrembo kwelikweli na ni mama anayejitambua hivyo hafikirii kuachana naye.  Van anasema haachani naye leo wala kesho licha ya kuwa kuna baadhi ya watu wanatamani penzi lao livunjike hata kesho.

Yes! Si mwingine, hapa namzungumzia Fahyma binti mwenye umri mdogo lakini mkubwa kifikra, Showbiz Xtra ilifanikiwa kufanya naye mahojiano ambapo alifunguka mambo mengi usiyoyajua ikiwemo ishu ya kufunga ndoa na Rayvanny. Enjoy mahojiano kamili hapa chini:

Showbiz: Mambo Fahyma, umepotea sana siku hizi, huonekani kabisa ukishiriki kwenye video za wasanii kama ilivyokuwa zamani, vipi u-video vixen haulipi nini?

Fahyma: Hapana, siyo kama nimepotea, nipo ila kuna kitu kimoja ambacho watu hawakijui toka kwangu, mimi siyo video vixen na wala sijawahi kuwa, pia nachukia sana mtu akinitambulisha mimi kama video vixen, hivyo naomba watu waache kabisa kuniita mimi hivyo.

Showbiz: Lakini umewahi kuonekana kwenye nyimbo mbili ukiwa kama video vixen, wimbo wa Kwetu na Siri.

Fahyma: Ndiyo nimewahi kuonekana kwenye hizo nyimbo lakini nilifanya vile kwa sababu ya mume wangu (Rayvanny) nilimsaidia mume wangu, hizo video sijalipwa hata senti tano ila niliamua tu kumsaidia, lakini siyo kwamba hiyo ndiyo kazi yangu, hapana nilifanya kwa heshima ya mume wangu tu kwa sababu yeye ndiye alinitaka mimi kuwa kwenye video zake.

Showbiz: Sasa unajishughulisha na nini? Maana tumezoea tu kukuona mitandaoni ukitupia picha zako.

Fahyma: Unajua mimi nafanya mambo mengi sana ambayo watu wengi hawawezi kuyafanya, lakini huwa sipendi kuyaanika hadharani, hata mume wangu analijua hilo, anafahamu kuwa sipendi mambo yangu kila mtu ayajue lakini ukweli ni kwamba mimi nina plan za kufungua kitu flani kuhusiana na mambo ya mavazi, pamoja na urembo, hivyo Mungu akijaalia hivi karibuni nitakuja na ‘product’ yangu mwenyewe ambayo itakuwa ni brand yangu.

Showbiz: Ok, nimeona una foundation yako inaitwa Fahyvanny- Empower- Foundation, idea ya hiyo kitu uliitoa wapi na kwa nini uliamua kufanya hivyo?

Fahyma: Mimi huwa nasaidia watoto yatima na watu wasiojiweza kila siku, hata hivi vituo vya watoto yatima wananijua, ila huwa sipendi kujitangaza sana kama nilivyosema hapo mwanzo, hivyo nikaona kuna haja ya mimi kuanzisha foundation yangu ambayo itasaidia watu wengi wenye matatizo mbalimbali hapa nchini kwetu ndipo nikaanzisha hiyo.

Showbiz: Hiyo foundation itakuwa ni endelevu au ni ya muda mfupi tu?

Fahyma: Hapana hiki ni kitu endelevu lakini kwa sasa hivi bado kuna vitu havijakamilika sana kwenye hiyo foundation ndiyo maana sija-expose sana lakini itakapokamilika nitai-expose, ila mimi ni mtu ambaye kila siku iendayo kwa Mungu nasaidia sana watu, anapotokea mtu ana shida namsaidia pale ninapoweza.

Showbiz: Hongera kwa kufanikiwa kuwa nominated kwenye tuzo za Starqt.

Fahyma: Nashukuru sana.

Showbiz: Tuambie ilikuwaje wakakuchagua wewe na ni vigezo gani ambavyo waliviangalia?

Fahyma: Kwanza kabisa wao ndio walianza kunitafuta mimi na wakaniambia nimekuwa nominated kwenye Tuzo za Best Dressed Lady ambazo zinatarajia kuanza Agosti, mwaka huu pia kuhusu vigezo wanaangalia tu jinsi mtu unavyojiweka na jinsi unavyojipangilia kimavazi.

Showbiz: Huonekani ukishawishi sana mashabiki zako mitandoni ili wakupigie kura kwa nini?

Fahyma: Itakapofika hiyo Agosti ndiyo tutaanza kuhamasisha watu, pia nitaomba Watanzania wanisaidie ku-vote, lakini sasa hivi tumeweka tu hadharani ili watu wajue na waone.

Showbiz: Makao makuu ya Starqt Awards yapo Johannesburg, Afrika Kusini, vipi utaenda kushiriki siku ya tukio ikifika?

Fahyma: (Anacheka) Ndiyo nitaenda naomba sana Mungu aniwezeshe kwa hilo.

Showbiz: Ulijisikiaje siku ambayo walikutafuta na kukuambia kuwa umekuwa nominated?

Fahyma: Nilijisikia vizuri sana, pale ndio nikajua kuwa ahaa kumbe watu wananiona hivyo naamini ndoto zangu zinaenda kutimia.

Showbiz: Kuna kipindi uliandika maneno kwenye akaunti yako kuwa wewe na Rayvanny tayari mmeshafunga ndoa, hivyo ni mume wako halali lakini kitu ambacho mnakisubiri sasa hivi ni sherehe tu, je ni kweli au uliamua tu kufanya hivyo kwa lengo la kuwakomesha wanaofuatilia penzi lenu?

Fahyma: Ni kweli mimi na Rayvanny tayari tulishafunga ndoa, ila bado tu kufanya sherehe, nadhani hicho kitu watu hawakijui ndiyo maana nikaandika vile kwenye akaunti yangu ili watambue na waache kuzungumza mambo wasiyoyafahamu.

Showbiz: Sasa Fay sherehe itakuwa lini?

Fahyma: Sherehe siwezi kuitaja itakuwa lini, lakini ikiwa tayari kila mtu atajua kwa sababu nitaweka wazi haitakuwa siri tena.

Showbiz: Tunajua kuwa wewe ni Muislamu na baba wa mtoto wako ni Mkristo, umebadili dini au kila mtu amebaki na dini yake?

Fahyma: Of course nimebadili dini, kwa hiyo sasa hivi mimi ni Mkristo.

Showbiz: Vipi una mpango wa kuongeza mtoto wa pili?

Fahyma: Ndiyo nina huo mpango tena natamani kuzaa hata kesho.

Comments are closed.