The House of Favourite Newspapers

Fedha za Yondani zazuia usajili Yanga SC

KOCHA Mkuu wa Yanga, Mwinyi Zahera ameuambia uongozi wa timu hiyo kuwa hawezi kufanya usajili wa wachezaji wapya kwenye dirisha dogo kwa kuwa wachezaji wake wengi bado wanadai fedha zao za usajili.

 

Zahera mwenye uraia wa DR Congo na Ufaransa ameyasema hayo kufuatia beki wake wa kati, Kelvin Yondani na kipa Beno Kakolanya kugomea kujiunga na timu kufuatia kudai fedha kwenye timu hiyo.

 

Yondani na Kakolanya wamegomea kujiunga na timu wakitokea kwenye kambi ya timu ya taifa, Taifa Stars kuelekea kwenye mechi mbili za Kanda ya Ziwa ambazo zote Yanga ilifanikiwa kushinda.

 

Akizungumza na Championi Jumatano, Zahera alisema kuwa hawezi kufanya usajili wa wachezaji wapya katika usajili wa dirisha dogo iwapo viongozi wa timu hiyo watashindwa kumaliza matatizo ya wachezaji waliopo kwa sasa kwenye kikosi chake.

 

“Kama ukimya basi fahamu kuna tatizo, unajua usajili ni kitu kikubwa, unaweza nyumbani kukawa na matatizo, mtoto wako haendi shule sasa sijui kama unaweza tena kuleta mtoto wa kaka au dada yako ukasema aje akae katika mazingira ya matatizo, siyo sawa.

 

“Sasa hapo ukiangalia unaona kuna shida, siwezi kusajili wachezaji wapya wakati tayari kuna wachezaji wasiopungua kumi bado wanadai fedha zao za usajili, nimeuambia uongozi kama hawatekelezi kumaliza matatizo ya wachezaji hauwezi kusajili wapya wakati wa zamani bado wana matatizo.

 

Kocha huyo aliendelea kufafanua kwa kusema kuwa: “Nina wachezaji kumi wamekuja kuniona kila mmoja akisema kwamba wakati anasaini uongozi ulimpa ahadi lakini mpaka sasa hajaona chochote, sasa sitafuti wapya wakati wengine wananililia kocha! kocha, haiwezekani na kama uongozi hautekelezi haya ya wachezaji basi nitaendelea na hawa,” alisema kocha huyo.

Ibrahim Mussa, Dar es Salaam

MKWASA Ampa Somo Zito AMUNIKE Ataja FIGISU TAIFA STARS

Comments are closed.