The House of Favourite Newspapers

FEI TOTO: MSIKATE TAMAA, UBINGWA WETU HUU

KIUNGO mchezeshaji fundi, Feisal Salum ‘Fei Toto’, amesema kupoteza mchezo wao wa juzi ni sehemu ya matokeo huku akiahidi kuendelea kupata matokeo katika michezo ijayo ya Ligi Kuu Bara hadi watwae ubingwa wa ligi hiyo.

 

Yanga juzi ilipoteza mchezo wake wa ligi baada ya kufungwa na Simba bao 1-0 ambalo limefungwa na Mnyarwanda, Meddie Kagere kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, Fei Toto alisema Simba walitumia vyema nafasi moja waliyoipata na kufanikiwa kupata ushindi huo walioupata.

 

Fei Toto alisema hawajakatishwa tamaa na matokeo hayo waliyoyapata ya kufungwa na Simba na badala yake wataendelea kupambana kuhakikisha wanafanya vizuri katika michezo inayofuata ya ligi.

 

Fei Toto alisema, walijipanga kwa ajili ya ushindi katika mchezo huo, lakini bahati haikuwa yao wakaambulia kipigo hicho walichokipata.

 

“Tulijipanga vizuri, tumepoteza mchezo kama sehemu ya matokeo tu, kama mchezaji au shabiki lazima ukubali kuwa mpira una matokeo matatu, kufungwa, kushinda na droo.

 

“Mungu kawajalia Simba wamepata ushindi, tunawapongeza katika hilo, kikubwa tunajipanga kwa ajili ya michezo ijayo ya ligi na kikubwa tunataka

kuona timu ikiendelea kuongoza ligi na mwishoni mwa msimu tuchukue ubingwa.

 

“Hatukati tamaa, tutaendelea kupambana, niwaombe mashabiki waendelee kutusapoti ili tupate matokeo mazuri,” alisema Fei Toto.

 

Kikosi cha Yanga kinatarajiwa kuelekea mkoani Mwanza kuikabili Mbao FC katika mchezo mwingine wa ligi utakaopigwa keshokutwa Jumatano kwenye Uwanja wa CCM Kirumba.

Comments are closed.